Kichuya arejea nchini kusaka timu


Mchezaji Ramadhan Kichuya amemaliza mkataba wa miezi sita na timu aliyokuwa anaichezea Misri, kwa sasa yupo nchini huku wasimamizi wake wakiendelea kuangalia wapi ataelekea.

Haya ndio yalikuwa majibu ya Kichuya baada ya kuulizwa kama atacheza vilabu vya hapa nyumbani kwa msimu ujao.

"Hakuna kisichowezekana kwenye maisha na mkataa kwao mtumwa, siwezi kusema sitaki kurudi nyumbani lakini kwa sasa malengo yangu ni kusonga mbele si kurudi tena nyuma."

Aliendelea kwa kusema, "Unaporudi nyuma unatakiwa kufanya kazi kubwa kurudi pale ulipokuwa lakini kama itashindikana inawezekana ukarudi na kujipanga ili kurudi ulipokuwa au zaidi ya ulipokuwa lakini lengo kubwa ni kupata changamoto nje ya Misri na Tanzania."