Paul Pogba awagomea waandishi wa habari

Mchezaji ghali zaidi kwenye kikosi cha Manchester United Paul Pogba amegoma kuongea na waandishi baada ya timu yake kuifunga Perth Glory ta Australia 2-0.

Mchezo huo ni wa kwanza kwa United katika kampeniyake ya kujiandaa na msimu ujao wa ligi.

Magoli ya ipindi cha pili kutoka kwa Marcus Rashford na James Garner yalitosha kwa Man United kutoka na vicheko kwenye uwanja wa Optus nchini Australia.

Pogba alitoa pasi iliyozaa goli la Rashford.

Huu ulikuwa mchezo wa kwanza kwa Pogba akiwa na United toka alipotangaza nia yake ya kutaka kuondoka kwenye kikosi hicho.

Nia hiyo ya Pogba imesharejelewa mara mbili na wakala wake Mino Raiola katika siku za hivi karibuni.

Kiungo huyo aligoma kuongea na maripota baada ya mchezo akisema "hakuna haja" ya kufanya hivyo.

Vilabu vya Real Madrid na Juventus vinaripotiwa kutaka kumsajili kiungo huyo Mfaransa mwenye miaka 26 japo hakuna kati yao ambaye amepeleka maombi rasmi ya kutaka kumnunua.

United inaaminika itataka kulipwa pauni milioni 150 ili kumuachia Pogba aende zake.

Pogba hakupewa kitambaa cha unahodha kwenye mchezo huo na kuvaliwa na Juan Mata, japo kocha wa United Ole Gunnar Solskjaer alisema kabla kuwa mchezaji huyo anaweza kupewa majukumu ya unahodha msimu huu.

"Sidhani kama jambo hilo linahitaji kutolewa maelezo, tutalijadili baadae," alisema Solskjaer alipoulizwa kuhusu hatima ya unahodha kwa Pogba.

Kuhusu uhamisho, Solskjaer amesema kuwa klabu hiyo haijapokea ofa yoyote ya wanaomtaka Pogba ama mshambuliaji wa Ubelgiji Romelo Lukaku, "tusubiri kuona msimu utakavyoanaza," alisisitiza Solkjaer.