https://monetag.com/?ref_id=TTIb Simba SC na Yanga SC wazidi kuandamwa na CECAFA | Muungwana BLOG

Simba SC na Yanga SC wazidi kuandamwa na CECAFA


Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholaus Musonye amezijia juu kwa mara nyingine klabu za Simba na Yanga kufuatia kutohudhuria michuano ya Kagame Cup iliyomalizika hapo jana.

Akizungumza baada ya fainali ya Kagame Cup kati ya Azam FC na KCCA ya Uganda, Musonye ameendele kusisitiza kuwa kutokuwepo kwa klabu za Simba na Yanga hajaathiri chochote katika michuano hiyo, akisema kuwa klabu hizo ziachwe ziendelee kuzunguka nchi za wengine huku zikiacha mashindano kwenye ukanda wao.

"Nawaambia Simba na Yanga kwamba hata kama hawakuja watambue sisi hatukumuomba mtu, tuna timu nyingi sana za kujaza nafasi hizo. Wao waende huko Afrika Kusini, Uturuki wakaangalie majumba na takataka zingine zilizopo huko", amesema Musonye.

"Kwanza kuna pre-season gani nzuri ambayo walitakiwa kuwa nayo zaidi ya hii?, yaani unaogopa kushindana, unakwenda kucheza mechi za kirafiki ambazo hazina maana. Serikali ya Rwanda imeandaa kila kitu hapa imesema njooni mcheze, wewe hutaki unakwenda Afrika Kusini kutembea", ameongeza.

Michuano ya CECAFA Kagame Cup imemalizika rasmi jana kwa mchezo wa fainali kupigwa, ambapo KCCA ya Uganda imefanikiwa kunyakuwa ubingwa kwa kuifunga Azam FC bao 1-0. Katika mchezo wa mshindi wa tatu, Green Eagles imeshinda kwa 2-0 dhidi ya AS Maniema Union.