Venezuela yawatia mbaroni walinzi wawili wa kiongozi wa upinzani

Mamlaka nchini Venezuela zimewatia mbaroni walinzi wawili wa kiongozi wa upinzani, Juan Guaido, kwa tuhuma za kujaribu kuuza silaha za nchi.

Mkuu wa chama cha kisoshalisti, Diosdado Cabello, amesema kwamba walinzi hao wawili, walipanga kuuza silaha zinazodaiwa kutumiwa wakati wa jaribio la uasi wa kijeshi mwishoni mwa mwezi Aprili.

Naye Waziri wa Habari Jorge Rodriguez alisema hatua ya kutaka kuuza silaha wakati majadiliano yakiendelea, kunaashiria udanganyifu kutoka upinzani.

Guaido aliandika katika ukurasa wa Twitter kwamba walinzi wake wawili wamekamatwa mjini Caracas wakati walipokuwa wakilinda familia yake, mnamo wakati yeye mwenyewe alikuwa amesafiri nje ya mji.

Kukamatwa huko kunatokea huku wawakilishi wa serikali ya Venezuela na upinzani wakijaribu kutafuta ufumbuzi wa mkwamo wa kisiasa chini ya usimamizi wa Norway.