Vijana Kilosa watoa heko kwa Rais Magufuli kurejesha Ardhi mikononi kwa Wananchi

Vijana wa Kata ya Msowero,Wilaya ya Kilosa,Mkoani Morogoro wamemshukuru na kumpongeza Mh Rais Dr John Pombe Magufuli kwa hatua yake madhubuti ya kufuta hati za mashamba makubwa yaliyokuwa yanamilikiwa na watu wachache na kuyarejesha mikononi mwa wananchi kwa matumizi ya Umma ambapo maamuzi hayo yamewanufaisha Vijana wa Kata ya Msowero kwa kupata ekari 300 za Kilimo cha Mpunga.

Hayo yamesemwa leo Wilayani Kilosa mbele ya Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Vijana na Ajira Mh Anthony Mavunde wakati wa mavuno ya Mpunga katika Shamba la Mpunga linalomilikiwa na Vijana wa Kampuni ya Agri-Ajira ambao ni wahitimu wa Chuo cha Kilimo Sokoine.

Wakisoma Risala yao Wakurugenzi wa Kampuni hiyo Bw Ibrahim Charles na Bw. Samson wameishukuru Serikali ya Rais Magufuli kwa kuwapatia eneo la kilimo la ekari 50 chini ya uratibu wa Mkuu wa Mkoa Dr Stephen Kebwe na Mkuu wa Wilaya Mh Adam Mgoyi,na hivyo kuiomba Serikali iwaongezee eneo kubwa zaidi la ekari 500 ili kupanua kilimo chao na kuongeza nafasi za Ajira kwa Vijana kutoka 200 kwa sasa mpaka kufikia 1000  na pia serikali iwawezeshe kuboresha miundombinu ya umwagiliaji ili wafanye kilimo bora na chenye tija.Vijana hao wlishindwa kuzuia hisia zao kwa kutokwa na machozi katika kuonesha shukrani zao kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Vijana ya Petrobena East Africa Ltd Ndg Peter Kumalilwa kwa msaada mkubwa aliowapa mpaka kufika hapo walipofika kwa ushirikiano wa Wakala wa Mbegu (ASA) kutoka Wizara ya Kilimo.

Akijibu Risala hiyo Naibu Waziri Mavunde amewapongeza Vijana wa Agri-Ajira Co.Ltd kwa kazi kubwa waliyoifanya mpaka kufiki mafanikio makubwa siku ya leo ya mavuno ya mpunga,na kwamba Serikali itawawezesha kimtaji kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB)ili kupanua kilimo chao zaidi na kutoa Fursa zaidi ya Ajira kwa Vijana na kumtaka Afisa kutoka Benki ya Kilimo kutoondoka hapo Shambani leo ili waweke sawa andiko la mkopo na mahitaji ya Vijana kutoka Benki ambapo Benki hiyo imeonesha utayari wa kusaidia mtaji zaidi kwa Kampuni hii ya Vijana.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi,Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Mh Adam Mgoyi amewahakikishia Vijana wa Kilosa kwamba Serikali itakuwa nao bega kea bega hasa katika kuwapatia maeneo ya kilimo ili kuongeza uzalishaji wa mazao yatokanayo na kilimo wilayani humo na kuahidi kulifanyia kazi haraka ombi la ekari 500 za ziada zilizoombwa na Kampuni hiyo ya Vijana.