Jukwaa Huru latinga kwa DC Jokate, watoa taulo za kike

Uongozi wa Jukwaa Huru la Wazalendo nchini wametembelea uongozi wa wilaya ya Kisarawe chini ya DC Jokate Mwogelo na kumkabidhi mchango wa boksi 10 za taulo za kike kama sehemu ya kusapoti program maalum ya tokomeza ZERO wilaya ya kisarawe.

Akizungumza baada ya kukabidhi taulo hizo Mwenyekiti wa Jukwaa hilo, Gertrude Ndibalema amesema lengo la ziara hilo ni kupongeza juhudi kubwa ambazo zimekua zikifanywa na DC Jokate katika kuongeza ufaulu kwa wilaya hiyo na hasa kuwainua watoto wa kike.


Amesema Jukwaa huru la wazalendo limekua likihamasisha uzalendo kwa Watanzania na hasa vijana ndani ya Nchi yao kwa kuwa wanatambua ili Taifa lolote liwe salama ni lazima liwe katika mikono salama ya kiuongozi.

" Jukwaa letu limekua likihamasisha uzalendo na tunafahamu ili Nchi iwe salama ni jukumu letu sisi vijana wa kizazi cha sasa kutoa hamasa kwa Watanzania wenzetu kuipenda Nchi yao, kusapoti kazi kubwa inayofanya na viongozi wao haswa Rais Dk John Magufuli na wasaidizi wao," amesema Ndibalema.

Pia amesema Jukwaa lao limejipanga kurudisha misingi ya kiuzalendo iliyoasisiwa na Baba wa Taifa hayati Mwalimu Nyerere ili vijana waweze kutambua nini maana ya uzalendo.

" Misingi ya TANU ni pamoja na kuipenda Nchi yako, hivyo kufika kwetu hapa Kisarawe kwa DC Jokate ni kuonesha  jinsi gani tuna uzalendo na Nchi yetu na tutatoa sapoti yetu kwa viongozi wetu ambao wamekua na maono ya kiukombozi kwa wananchi wanaowatumikia," amesema Ndibalema.

Kwa upande wake DC Jokate ameupongeza uongozi wa Jukwaa hilo kwa namna ambavyo wamekua wakijitoa katika kuitumikia Nchi yao na kushirikiana na Serikali Katika kuijenga Tanzania ambayo ina lengo la kufikia uchumi wa kati.

" Mimi niwashukuru sana kwa kufika wilayani kwetu, hichi mlichokifanya leo historia itawakumbuka, niwaahidi kuwapa ushirikiano wa hali na Mali katika jambo lolote la kimaendeleo ambalo mtahitaji uwepo wangu, ninawashukuru sana na ninaomba mtumie Jukwaa lenu katika kuhamasisha na kuwa daraja la kiuzalendo kati ya vijana na Serikali yao," amesema DC Jokate.