MNEC Mwakitinya atoa neno zito kwa vijana wa CCM

Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mussa Mwakitinya amewataka vijana wa Chama hicho kusimama mstari wa mbele kumtetea Rais Dk John Magufuli kwenye mitandao ya kijamii.

Mwakitinya ameyasema hayo wakati akizindua mashina ya wakereketwa wa Umoja wa Vijana 13 katika matawi saba ya Kata ya Mbagala Kuu Wilaya ya Temeke Jijini Dar es Salaam.

" Rais Magufuli anafanya mambo ambayo sisi wote hatukuwahi kutegemea yatafanywa Tanzania, Elimu bure, Nidhamu kwa watumishi, ujenzi wa reli ya kisasa na bwawa la kufua umeme, mtandao wa barabara za lami Nchi nzima, na zaidi ujenzi wa Tanzania ya uchumi wa viwanda, tusimame kumtetea Rais wetu dhidi ya watu wasioitakia mema Nchi yetu, " amesema Mwakitinya.

Katika ziara hiyo Mwakitinya aliambatana na Aliyekua Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Vijana Chadema Taifa, Gertrude Ndibalema ambaye alijiunga na CCM ambapo nae alitumia nafasi hiyo kuwataka vijana kuwa mstari wa mbele katika kuhubiri mambo makubwa yanayofanywa na Rais Magufuli.

" Sisi ndio msingi wa Maendeleo katika Taifa letu, Serikali ya CCM chini ya Dk Magufuli imeonyesha dira kwa Taifa letu ni jukumu letu kumsemea vizuri Mwenyekiti ambaye pia ndio Rais wetu, tusiogope twendeni mbele na kueleza yale yote mazuri yanayofanywa na Serikali yetu," amesema Ndibalema.