Mume amkata mke mikono kwa madai ya kutozaa


Mama mmoja chini Kenya amekatwa mikono yote miwili na mumewe kwa kutumia kisu akidai kwamba ameshindwa kumzalia watoto, katika kile kinachosemekana ni tukio baya zaidi la ugomvi wa nyumbani.

Mama huyo ambaye ni Jackline Mwende mkaazi wa kijiji cha Kathama, Kaunti ya Machakos amedumu katika ndoa na mume wake huyo kwa miaka saba.

Mikono yake ilikatwa kutoka katika kifundo cha mkono na mumewe Stephen Ngila Thenge na pia ana majeraha kichwani na shingoni kutokana na shambulio hilo Julai 24 mwaka huu.

Ndugu zake wamesema kuwa wanandoa hao walikuwa na matatizo na kwamba bi Mwende alitaka kumwacha mumewe, lakini akashauriwa kutofanya hivyo na kiongozi mmoja wa dini.

Mwende amesema kabla ya shambulio hilo, walikuwa wakiishi mbalimbali na mumewe kwa takriban miezi mitatu kwa kosa la kutopata watoto.