Rais Ali Bongo ajitokeza hadharani kuhuduria sherehe za uhuru

Rais wa Gabon Ali Bongo hii leo amejitokeza hadharani kuhuduria sherehe za uhuru wa nchi hiyo, ikiwa ni takriban miezi 10 tangu augue kiharusi.

Hali yake ya afya ilizua masuali mengi juu ya uwezo wake wa kuongoza taifa lake. Bongo ambaye kila hatua anayopiga inachunguzwa kujua anavyoendelea kiafya, hapo jana Ijumaa alishiriki tafrija kadhaa za kuadhimisha uhuru wa Gabon kutoka kwa Ufaransa.

Gabon ilipata uhuru wake mnamo mwaka 1960. Leo Jumamosi Rais Ali Bongo alihudhuria gwaride la kijeshi katika mji wa pwani wa Libreville.

Mashaka ya iwapo Bongo anaweza kuliongoza taifa hilo dogo tajiri kwa mafuta yalitokea baada ya kuugua kiharusi akiwa Saudi Arabia.

Alisafirishwa kwa ndege hadi Morocco kwa matibabu zaidi na kurejea nchini Gabon mwezi wa Januari. Wakati alipougua jeshi lilizima jaribio la mapinduzi nchini humo.