https://monetag.com/?ref_id=TTIb Rais Mstaafu Mkapa asisitiza dhamira ya dira ya SADC | Muungwana BLOG

Rais Mstaafu Mkapa asisitiza dhamira ya dira ya SADC


Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) inatakiwa kukumbuka na kurejea kwenye Dira na Dhima za Jumuiya hiyo ili kuweza kuimarisha, kuongeza na kuwezesha ushirikiano wa nchi za kusini mwa Afrika kuwa katika lengo moja na kusonga.

Hayo yalisemwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Tanzania Benjamin Mkapa alipokuwa akizungumza katika mhadhara wa wajumbe na viongozi wa SADC katika Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Rais Mkapa alisema kuwa katika kujenga uchumi ulioimara nchi hizo zinatakiwa kukumbuka Dira na Dhima ya kuanzishwa kwa Jumuiya hiyo ya nchi za Kusini mwa Afrika ili kuweza kuimarisha uchumi ulioendelevu; wenye kuwezesha wananchi kutoka nchi wanachma kuwa na maisha bora.

“Naamini kuwa SADC imeweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kwenye muundo wa Maendeleo ya Bara la Afrika, na suala hili linapaswa kutangazwa ili ushirikiano huu uendelee kwa wananchi wanachama wa SADC, lakini haya yote yamesababishwa na kuwa na Dira na Dhima ambayo inaruhusu nchi hizi kuwaza na kutekeleza mawazo yao pamoja”, alisema Mkapa.

Kiongozi huyo Mstaafu alisema kuwa SADC inatakiwa kukumbuka Dira ya kuanzishwa kwa Jumuiya hiyo ambayo ni kuunganisha na kuhusianisha Utumiaji wa rasrimali zilizoko nchi wanachama ili kuwezesha nchi hizo kujitegemea na kuimarisha uchumi wake pamoja na maisha ya watu wake.

Mkapa alifafanua kuwa Dira hiyo inapaswa kutekelezwa huku nchi wanachama wakikumbuka waasisi wa SADC akiwemo Baba wa Taifa, Hayati Julius Nyerere kuwa ilikuwa ni kuungana nakufanya kazi kwa pamoja ili kulinda rasrimali na kuwezesha wananchi kujitegemea kwa kuisha maisha yaliyobora.

Aidha, Mkapa alisema kuwa SADC ina dhima kubwa ya kuendeleza uchumi endelevu na ulio sawa kwa nchi wanachama kupitia mifumo mizuri, utawala bora na kuongeza ushirikiano wa nchi hizo, na vitu hivyo vitawezesha upatikanaji wa amani na usalama kwa nchi wanachama pamoja na ujenzi wa miradi mbalimbali ya ushirikiano.

“Dira ya SADC ni moja na nguzo muhimu katika utekelezaji wa miradi ya Maendeleo ikiwemo miradi ya Nishati, Miundombinu ya usafarishaji na ujenzi wa viwanda hii yote ni utekelezaji wa kuifanya SADC kuwa katika uchumi ulio sawa ukanda huu wa nchi za kusini mwa Afrika”, alisema

Aliongeza kuwa Miundombinu ya nchi za Afrika inatakiwa kuimarishwa kama mkakati wa nchi za SADC unavyoeleza, kwa sasa SADC inatakiwa ijikite katika ujenzi wa Viwanda na Nishati ambapo vitu hivyo vikitekelezwa SADC itasonga mbele.

Kwa upande wake Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Namibia, Natumbo Nandi Ndaitwah, alisema kuwa Jumuiya ya SADC inapaswa kuzingatia kumbukumbu ya kuasisiwa kwake ili kuweza kusonga mbele katika mashirikiano ya pamoja kwa nchi hizi.

Waziri Ndaitwah alisema kuwa kumbukumbu ya Waasisi wa SADC itakumbukwa milele huku akiitaja Tanzania kuwa ni moja ya Taifa ambalo limeweza kusaidiwa kwa kiasi kikubwa katika ukombozi wa Afrika na kundwa kwa jumuiya hiyo.

“Nchi wanachama wa SADC tunapaswa kujua kuwa Tanzania ni taifa ambalo limewezesha kwa kiasi kikubwa kuzaliwa kwa Jumuiya hii, kwani Mwl. Nyerere aliwezesha nchi nyingi za upande wa Kusini mwa Afrika kukombolewa na alikuja na wazo la kuunda Jumuiya ya SADC ili nchi za kusini zipate kufanya kazi pamoja na kuimarisha maisha ya watu wao”, Naibu Waziri Mkuu, Ndaitwah.

Waziri Ndaitwa alisema kuwa Mwl.Nyerere ni mfano wa kuigwa kwa nchi wanachama wa SADC na anapaswa kubaki katika kumbukumbu ili vizazi vijavyo viweze kukumbuka kuwa kuna Mwanzilishi na mkombozi wa Nchi za Kusini mwa Afrika.

“Namshukuru Baba wa Taifa, Mwl.Julius Nyerere, aliyetangaza kuwa, Tanzania haiwezi kuwa huru kama Bara la Afrika halijakombolewa, nayasema haya ili tujue tulikotoka na nani alifanya kitu gani ili tuweze kusonga mbele katika Jumuiya hii ya Nchi za Kusini mwa Afrika”, Naibu Waziri Mkuu, Ndaitwah.