DC Mpogolo aagiza wahandisi kutoa ushauri wa kitaalamu kwenye miradi ya maendeleo

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Edward Mpogolo amewataka wahandisi wa Wilaya hiyo kuhakikisha wanatoa ushauri katika kila mradi unaojengwa kwa nguvu za wananchi.

DC Mpogolo amesema ni jambo la kushangaza kuona wananchi wanamuunga mkono Rais Dk John Magufuli kwa kushirikiana na Serikali kujenga miradi mbalimbali halafu hawapati ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wahandisi.


Hayo ameyasema wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi anayoifanya kwenye Wilaya hiyo.


DC Mpogolo amesema toka ameanza ziara hiyo na kukagua baadhi ya miradi inayojengwa kwa nguvu za wananchi vikiwemo vyumba vya madarasa hakuna sehemu yeyote ambayo wahandisi wamefika na kutoa ushauri wao.

" Hakuna mradi wenye nguvu za wananchi ambao watalaamu letu wamefika na kutoa ushauri. Hivyo nawaagiza kutoka ofisini na kuja huku kushauri kuliko Wananchi wanatumia nguvu na kidato chao halafu watumishi wanaopaswa kuwahudumia wao wamekaa tu ofisini.


" Nimepita kwenye mashule, zahanati kote huko watalaamu hawajafika, wanasubiri fedha zinazotoka juu kwa kuwa zina posho hii wanaiacha kwa kuwa haina posho, sasa natoa agizo na litekelezwe," Amesema DC Mpogolo.

Aidha amewataka wataalamu hao kupita kwenye miradi yote iliyopo kwenye Kata za Wilaya hiyo na kumletea ripoti inayoonesha miradi waliyoitolea ushauri.