Iran haitazungumza na Marekani - Khamenei

Kiongozi Mkuu wa Kidini nchini Iran, Ayatollah Ali Khamenei amesema " Hakutakuwa na mazungumzo ya ngazi yoyote na Marekani"-kauli ambayo inamaanisha, kuondosha dhana ya uwezekano wa kufanyika mkutano kati ya marais wa mataifa hayo mawili katika Umoja wa Mataifa baadae mwezi huu.

Televisheni ya taifa ya Iran imemnukuu Khamenei akisema huo ndio msimamo wa uongozi mzima wa taifa na maafisa wote katika Jamhuri hiyo ya Kiislamu.

Kumekuwa na taarifa zenye kueleza uwezekano wa kufanyika kwa mkutano kati ya Rais Donald Trump na mwenziwe wa Iran, Hassan Rouhani, wakati wa Hadhara Kuu ya Umoja wa Mataifa inayotarajiwa kufanyika mwezi huu mjini New York, Marekani.

Iran mara zote imeitaka Marekani kurejea katika makubaliano ya nyuklia ya mwaka 2015.

Tangazo la Iran limekuja wakati jana Jumatatu Trump alitangaza kwamba inaoenesha kama Iran ilikuwa nyuma ya shambulio la bomu dhidi ya eneo la viwanda vya mafuta vya Saudi Arabia.