TRC na DIT zatiliana saini makubaliano ya kukuza matumizi ya Teknolojia katika usafiri wa Reli


Shirika la Reli Tanzania – TRC limetiliana saini mkataba na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam – DIT kwa lengo la kushirikiana katika kutoa mafunzo, kufanya utafiti, na kuendeleza matumizi ya teknolojia katika huduma za usafiri wa reli, makubaliano yamefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Makao Makuu TRC jijini Dar es Salaam Septemba 11, 2019.

Makubaliano hayo yametiliwa saini kati ya Mkurugenzi Mkuu wa TRC Ndugu Masanja Kungu Kadogosa  na Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof. Preksedis Ndomba pamoja na wanasheria kutoka pande zote mbili ambapo hafla hiyo fupi imehudhuriwa na Wakuu wa Idara mbalimbali kutoka TRC, wawakilishi kutoka DIT na waandishi wa habari.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania ameeleza dhumuni la makubaliano hayo ni kuwa ni kutokana na mabadiliko yanayotarajiwaa kutokea katika Shirika hususani katika huduma, amesema kuwa  matumizi ya teknolojia ni muhimu kwa kuwa tayari Shirika linasimamia miradi mikubwa ukiwemo wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa – SGR, Uboreshaji wa Reli ya Kati – TIRP na ukarabati wa Mabehewa hivyo kuwa na wataalamu wa kutosha watakaoleta chachu katika matumizi ya teknolojia ni muhimu.

“TRC tuko kwenye mageuzi na mageuzi yanakuja na teknolojia na vitu vipya, tunajenga reli ya kisasa – SGR kwahiyo tunahitaji kujua mifumo ya uendeshaji jinsi ilivyo kwahiyo sisi tumelikaribisha hili,” alisema Kadogosa

Naye Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam amesema kuwa hatua hiyo imekuja ikiwa ni sehemu ya maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo alizitaka taasisi, Mashirika na serikali kufanya mageuzi ya teknolojia hivyo Taasisi hiyo ikaamua kuzishirikisha taasisi, serikali na makampuni katika kutoa mafunzo kwa wanafunzi wake, pia amesema kuwa TRC ni taasisi ya kimkatati kwa ajili ya kujifunza.

“Tunaiona TRC kwa ukubwa wake, umaarufu wake na historia yake ni darasa moja kubwa sana si kwa wanafunzi tu hata kwa wafanyakazi, TRC ni taasisi ya kimkakati ambavyo tunaweza kujifunza” alisema Prof. Ndomba