Wanaojenga katika hifadhi za barabara wapewa onyo kali


Na Ferdinand Shayo-Arusha

Diwani wa kata ya Olasiti Alex Marti ametoa onyo Kali kwa wananchi wanaojenga katika hifadhi za barabara na kukwamisha miradi ya ujenzi wa barabara na kuweza  kusababisha migogoro na kuzorotesha utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara.

Akizungumza katika mkutano na wananchi amesema kuwa wanaojenga kwenye hifadhi ya barabara wamekua wakiwavunja wahisani na wadau wa maendeleo wanaotoa fedha kwa ajili ya miradi hiyo.

Marti amesema kuwa licha ya mpango wa kuboresha miundombinu tayari serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Kibo kwa kiwango cha lami jambo ambalo litawasaidia wananchi.

"Tunaishukuru serikali ya Rais John Magufuli kwa kutoa fedha nyingi za kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu, ujenzi wa madarasa na shule" Alisema Diwani huyo

Aidha amewataka wananchi kushirikiana na serikali na kulinda miradi hiyo na kuhakikisha kuwa miundombinu haiharibiwi.