Zanzibar, Indonesia zaazimia kuendeleza ushirikiano


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza azma ya Serikali ya Indonesia ya kuja kuekeza Zanzibar kupitia Makampuni na Mashirika yake ya Umma kutokana na fursa zilizopo hapa nchini.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri anayeshughulikia Mashirika yanayomilikiwa na Serikali ya Indonesia Bi Rini Mariani Soemano.

Bi Rini Mariana amefuatana na ujumbe wake wa watu 30 akiwemo Balozi wa Indonesia katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Ratlan Pardede na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Malaysia ambaye pia, anaiwakilisha Tanzania nchini Indonesia Balozi Dk. Ramadhan Kitwana Dau.

  Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alimueleza Waziri Soemarno kuwa azma hiyo ya Serikali ya Indonesia ni hatua moja wapo ya kukuza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano ulioasisiwa na waasisi wa Mataifa hayo akiwemo Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Hayati Soekarno Hatta Baba wa Taifa la Indonesia.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kushirikiiana na Makampuni na Mashirika yote ya Umma ya Indonesia yalioonesha azma ya kuja kuekeza hapa Zanzibar katika sekta mbali mbali za maendeleo.

“Sisi ni wamoja na tuna urafiki na udugu wa damu ulioasisiwa na viongozi wetu hao ambao ni waasisi wa Mataifa hayo hivyo, ni vyema tukauimarisha kwa nguvu zetu zote uhusiano wetu na ushirikiano tulionao licha ya kuwa tuko mbali lakini bahari ya India ‘Ocean’ isitugawe”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein aliipongeza Serikali ya Indonesia kwa kuendeleza uhusiano na Ushirikiano huo uliodumu kwa miaka 55 hivi sasa, na kueleza kuwa Zanzibar ina fursa nyingi za uwekezaji sambamba na mazingira mazuri yaliyowekwa na Serikali kwa ajili ya wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa hatua hiyo pia ni miongoni mwa matunda na mafaniko yaliyotokana na ziara yake aliyoifanya nchini Indonesia mwezi Agosti mwaka jana 2018 ambapo alipata fursa ya kuzungumza na mwenyeji wake Makamo wa Rais wa nchi hiyo Muhammad Jussuf Kalla masuala mbali mbali ya maendeleo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa ujio wa Waziri Bi Rini Soemarno unaonesha mwanzo mzuri wa mashirikiano hayo katika kuendeleza sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo uwekezaji, biashara, utalii, kilimo, miundombinu na nyengienzo.

Rais Dk. Shein alieleza haja ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya utalii hasa ikizingatiwa kuwa nchi hiyo imepiga hatua kubwa katika masuala ya utalii huku akieleza jinsi watalii kutoka Indonesia wanaokuja kutalii Zanzibar wanavyongezeka kila mwaka.

Dk. Shein aliunga mkono mazungumzo ya Waziri huyo alieleeza jinsi Serikali yake itakavyoangalia suala zima la kuwepo kwa usafiri wa ndege kati ya Indonesia na Zanzibar kupitia Madagasca hatua ambayo pia, itakuza sekta ya utalii na biashara baina ya pande mbili hizo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza haja ya kuimarisha sekta ya biashara baina ya pande mbili hizo hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar na Indonesia zina historia ya biashara ikiwemo biashara ya zao la karafuu.

Dk. Shein pia, alitilia mkazo suala zima la kuimarisha uhusiano na ushirikiano kwa njia ya kutembeleana kwa azma ya kupanua wigo wa kimaendeleo kati ya viongozi na watendaji mbali mbali jambo ambalo limekuwa likienda vizuri hadi hivi leo.

Mapema Waziri anayeshughulikia Mashirika yanayomilikiwa na Serikali ya Indonesia Bi Rini Mariani Soemano alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Serikali ya Indonesia ya kuleta Kampuni na Mashirikia yake kuja kuangalia fursa za kuekeza hapa Zanzibar.

Waziri Soemarno alieleza kuwa mazingira ya Zanzibar yameshabihiana na yale ya Indonesia hivyo ni rahisi kuja kuekeza hasa ikizingatiwa vivutio kadhaa vilivyopo hapa Zanzibar sambamba na hatua zinazochukuliwa na Serikali kwa wawekezaji.

Waziri huyo alieleza kuwa Makampuni na Mashirika ya nchini Indonesia yamevutiwa zaidi na jinsi ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi wanavyowajali  wageni wakiwemo ndugu zao wa Waindonesia jambo ambalo limewapa faraja kubwa.

Aidha, Waziri huyo alitumia fursa hiyo kumpa Rais Dk. Shein salamu kutoka kwa Rais wa Indonesia Joko Widodo na  kusisitiza kuwa nchi hiyo itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza na kuimarisha sekta za maendeleo.

Waziri Soemarno ambaye amefuatana na ujumbe wa watu 30 wakiwemo viongozi wa Mashirika mbali mbali ya Umma yanayoshughulikia masuala ya reli, huduma za viwanja vya ndege, mafuta na gesi asilia, benki, fedha na sekta ya miundombinu alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Serikali yake ina hamu katika kutekeleza jambo hilo.

Pia, Waziri huyo alimueleza rais Dk. Shein kuwa katika ziara yake ya siku mbili hapa Zanzibar atakutana na viongozi mbali mbali wa Serikali ambao watajadiliana masuala mbali mbali ya ushirikiano katika sekta kadhaa zikiwemo miundombinu, fedha, Wakala wa Maji na Nishati (ZURA), kukutana na Waziri wa Fedha Balozi Mohammed Ramia Abdiwawa pamoja na kutembelea eneo linalotarajiwa kujengwa bandari ya mafuta na gesi huko Mangapwani.

Pamoja na hayo,  Waziri Soemarno alimueleza Rais Dk. Shein jinsi Serikali yake itakavyoliangalia kwa umakini zaidi suala la kukuza ushirikiano katika usafiri wa anga kati ya nchi hiyo na Zanzibar hasa ikizingatiwa kwamba tayari kuna safari za ndege kati ya Indonesia na Madagasca.

Waziri Soemarno alieleza kuwa Serikali ya Indonesia inathamini juhudi za waasisi wa Mataifa hayo na kuahidi kuwa uhusiano na ushirikiano utaendelezwa katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo za kiuchumi baina ya pande mbili hizo na kusukuma mbele maendeleo kwenye sekta ya bandari, fedha, viwanda, usafiri na miundombinu.