Jambazi sugu lauwawa na wananchi wenye hasira kali



Na Ezekiel Mtonyole, Chemba.

Mtu mmoja anayesadikika kuwa ni jambazi ameuawa na wananchi wenye hasira Kali katika Kijiji Cha Soya, Wilaya ya Chemba Mkoa wa Dodoma alipokuwa akijaribu kuiba kwenye duka la mmoja la mkazi wa Kijiji hicho.

Kwa mujibu wa taarifa za wananchi wa Kijiji hicho kulikuwa na watu wageni walioingia Kijijini hapo na usiku wa kuamkia leo ndipo wakajaribu kuiba kwenye duka hilo ambapo wawili walifanikiwa kukimbia na mmoja kuuawa na wananchi wenye hasira kali.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Polisi Gilles Muroto, alifika katika eneo la tukio hilo na kusisitiza wananchi kutoa taarifa za watu wanaoingia katika maeneo yao na kuwa tilia mashaka.

"Nimesikia watu hawa wameingia siku kama tatu zilizopita(wananchi wiki moja) na ninyi hamkutoa taarifa, toeni taarifa za watu wanaoingia katika maeneo yenu, pia mtu hawezi kuja kama hana mwenyeji" amesema Kamanda Muroto.

Aidha wananchi hao wameomba kupelekewa Askari katika kata hiyo kwani kwa Sasa imekuwa na idadi kubwa ya watu hivyo wameomba kupelekewa askari na kubainisha kuwa tayari makazi ya askari yameshaandaliwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma ameahidi kupeleka Askari katika kata hiyo na kuwaomba wananchi hao kuwapa ushirikiano askari hao na kushirikiana nao kuwafichua waharifu.