Jeshi la Polisi Tanzania laendelea kuimarisha ulinzi na usalama mradi wa SGR


Makamishna pamoja na Maafisa waandamizi wa Jeshi la Polisi Tanzania wafanya ziara katika Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa - SGR kipande cha Dar es Salaam - Morogoro  hivi karibuni Septemba  2019.

Lengo la ziara hiyo ni kuona namna ya kuimarisha ulinzi ili kuhakikisha Miradi mikubwa ya kimkakati ukiwemo mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa - SGR unalindwa na unakuwa salama.

Makamishna na Maafisa hao walipata fursa ya kuona maendeleo ya Mradi pamoja na kazi zinazoendelea za ujenzi wa Stesheni ya Dar es Salaam, Pugu na Soga, ujenzi wa Madaraja, tuta, vivuko,  utandikaji wa reli na baadae walitembelea kiwanda cha Mataruma kilichopo Soga mkoani Pwani.


Ziara hiyo imefanyika baada ya kikao kazi cha Makamishna na Maafisa waandamizi wa Jeshi la Polisi Tanzania ambapo Kamanda wa Jeshi la Polisi Nchini - IGP Simon Sirro aliwataka Makamishna na Maafisa hao kutembelea Miradi mikubwa ili kuimarisha mikakati ya ulinzi.

Akizungumza na Reli na Matukio Kamishna wa Polisi Utawala na Rasilimali Watu, Kamanda Benedict Wakulyamba amesema kuwa jukumu la jeshi la polisi ni kuhakikisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao pamoja na mali za serikali ikiwemo Miradi mikubwa ya kimaendeleo.

“Miradi hii mikubwa ambayo tuna jukumu la msingi la kuhakikisha inakuwa salama na endelevu, Wajibu wetu wa kwanza ni kuhakikisha kuwa kuna ulinzi wa kutosha,” alisema Kamishna Wakulyamba.

Kwa upande wake Kamishna Mwandamizi Msaidizi wa Madawa ya Kulevya Zanzibar Kamanda Kheriyangu Mgeni Khamis ametoa shukurani kwa Shirika la Reli Tanzania kwa kuwapa taarifa na maelezo ya kutosha kuhusu mradi huo na amesema kuwa lengo la ziara hiyo ni kuona jinsi ya kuboresha ulinzi na usalama katika maeneo ya mradi. 

“Tumekuja hapa kwenye iara hii kuona ili tutakaporudi tuweze kujipanga kimkakati kwa ajili ya ulinzi na usalama” Kheriyangu Mgeni Khamis Kamishna Msaidizi upande wa Madawa ya Kulevya

Naye Meneja Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa – SGR Dar es Salaam – Morogoro Mhandisi Machibya Masanja kwa niaba ya Shirika la Reli Tanzania – TRC amelipongeza Jeshi la Polisi Tanzania na ameongeza kuwa Shirika limeweka mifumo ambayo haitaruhusu reli kuhujumiwa kwa kuwa reli ya kisasa itaungwa na kuwa moja (Continous Welded Rail), itawekewa na kufungwa na vifungashio ambavyo si rahisi kwa mtu kufungua na kuhujumu reli.

“Tunalipongeza jeshi la polisi kwa kuona umuhimu wa mradi, mradi huu si wa TRC ni wa watanzania, jeshi la polisi lina nafasi kubwa ndani ya mradi kwa sababu wao ndio wataalam wa ulinzi, tumebadilishana mawazo juu ya mfumo wa ulinzi na usalama tulionao katika mradi, sisi kama wahandisi tumekidhi katika kuweka mifumo ya kuhakikisha reli haihujumiwi” alisema Mhandisi Machibya

Shirika linaendelea kuhamasisha taasisi, jumuiya, makampuni na wananchi kwa ujumla kutoa ushirikiano kwa kulinda miundombinu ya reli kwa sababu miundombinu hiyo ina manufaa kwa umma wa watanzania, hivyo jukumu la ulinzi na usalama wa Miradi na Miundombinu ya reli ni la kila mmoja wetu.