DC aeleza ushirikina unavyokwamisha maendeleo


Mkuu wa wilaya ya Ludewa mkoani Njombe Bwana Andrea Tsere amesema shughuli za maendeleo katika wilaya hiyo zinakwamishwa na uwepo wa imani za kishirikina na uchawi, hali inayomlazimu atumie muda mwingi kutatua migogoro inayotokana na imani hizo inayosababisha pia mauaji.

Akizungumza na wazawa wa wilaya hiyo wanaoishi  mjini Njombe amesema ili kuondokana na imani hizo wilaya imeweka mikakati itakayohakikisha kuwa kila mtoto wilayani humo anapata elimu.

Amesema kutokana na hali hiyo wilaya inataraji kujenga shule ya sekondari ya watoto wenye vipaji kufuatia wilaya hiyo kuwa chini kitaaluma kwa miaka minne mfululizo kwa ngazi ya mkoa na kitaifa.

Baadhi ya wananchi wa wilaya Ludewa wanaoishi mjini Njombe wamesema wako tayari kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo.