Watanzania wahimizwa kudumisha amani na upendo


Watanzania wamehimizwa kuendelea kudumisha amani iliyopo nchini kwa kujiepusha na matendo yanayoashiria uvunjifu wa amani, sambamba na kujenga mshikamano na upendo miongoni mwao bila kubaguana kwa namna yoyote ile.

Kauli hiyo imetolewa na mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakar Bin Zuberi Bin Ally, katika mkesha wa sherehe za Maulid zilizofanyika kitaifa katika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza ambapo amewataka watanzania kuendelea kudumisha amani iliyopo nchini kwa kuvumiliana na kupendana wakati wote ili kuwa mfano wa kuigwa kwa mataifa mengine

Awali  akizungumza kwa niaba ya masheikh wa mikoa ya Tanzania, Sheikh wa mkoa wa Arusha Shabani Juma amewasisitiza watanzania kudumisha amani na upendo, huku Sheikh wa mkoa wa Mwanza Hassan Kabeke akimpongeza sheikh mkuu wa Tanzania Abubakar Zuber kwa utayari wa kuleta sherehe za Maulidi mkoani Mwanza baada ya miaka 29 tangu zilipofanyika kwa mara ya mwisho mkoani humo mwaka 1990.

Akitoa salamu za serikali katika mkesha wa sherehe za Maulid kitaifa mkoani Mwanza, waziri mkuu Mhe.Kassim Majaliwa amelipongeza baraza kuu la waisalamu Tanzania ( BAKWATA ), kwa kuendelea kudumisha umoja baina ya waislamu na kuwapongeza kwa kutambua ushirikiano mwema na nchi jirani katika nyanja mbalimbali

Sherehe za Maulid ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwa mtume Mohammed S.A.W yapata miaka 1440 huko Makka, Saudi Arabia, ambapo kwa kalenda ya kiislamu ni tarehe 12 ya mfungo sita.

.