India: Mamia waandamana kupinga ubakaji wa wanawake

Wabunge wa India hii leo wametaka hatua zaidi zichukuliwe dhidi ya wahalifu wa genge la ubakaji na mauaji ya mwanamke wa miaka 27, wakati mamia wakiandamana nchi nzima wakitaka uchunguzi ufanyike.

Wanaume wanne walio na umri wa miaka 20, walikamatwa siku ya Ijumaa kuhusiana na makosa ya kumbaka na kumuua daktari wa wanyama karibu na mji wa kusini wa Hyderabad.

Mabaki ya mwili wa mwanamke huyo yalipatikana baada kutoweka siku ya Jumatano. Polisi wanasema mwanamke huyo alinyongwa kabla ya mwili wake kuchomwa.

Wabunge katika mabunge yote hii leo wameelezea wasiwasi wao juu ya uhalifu dhidi ya wanawake na usalama wao na kutaka adhabu kali kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa.

Wakati huo huo mamia ya waandamanaji wamekusanyika eneo la karibu na bunge mjini New Delhi, wakitaka uchunguzi wa haraka ufanyike kuhusiana na mkasa huo.