Watendaji watume watakiwa kusimamia majukumu yao kwa mujibu wa madai ya malalamiko kwa wananchi



Na Thabit Madai,Zanzbar.

Mwenyekiti wa Tume ya Haki za binaadamu na Utawala Bora, Jaji Mstaafu,  Mathew Pauwa Mhina aliwataka watendaji  wa Tume ya Haki za binaadamu na Utawala Bora kusimamia majukumu yao kwa mujibu wa madai ya  malalamiko kwa Wananchi . 

Hayo aliyasema huko kwenye Ukumbi wa Jengo la Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala bora lilioko Mbweni  Wilaya ya Magharibi B Unguja wakati alipokuwa akiwatambulisha Makamishna wapya walioteuliwa hivi karibuni na kukagua jengo lililofanyiwa matengenezo.

Alisema malalamiko na madai ya Wananchi hutokezea pale ambapo wamecheleweshewa malipo  kupunwa au kutolipwa kabisa fidia ya mali zao ili waweze kuzifanyia ufumbuzi kwa haraka. 

Aidha Mwenyekiti  huyo alisema iko haja ya wananchi kupewa elimu kwa kufanyiwa mikutano katika shehia zao ili kupata uelewa wa jinsi ya kutetea haki zao  kwa lengo la kupatiwa ufumbuzi wakati wanapopeleka malalamiko yao katika Tume hiyo.

“Wananchi iko haja ya kupatiwa elimu na kufahamishwa majukumu ya Tume hii ili waweze kupata uelewa wa sehemu gani ya kuyapeleka malalamiko yao na kuweza kupatiwa ufumbuzi”, alisema Mwenyekiti huyo.

 Aidha alisema Serikali inapofanya shughuli zake za maendeleo kama vile ujenzi wa miundombinu katika maeneo ya wananchi hujitokeza malalamiko mengi ya madai ikiwemo kucheleweshwa kwa malipo au kutolipwa kabisa fidia za mali zao.

Hivyo alisema pamoja na kazi ya kupokea na kuchunguza malalamiko Tume inaendelea kutekeleza shughuli nyengine kwa mujibu wa sheria  kwa kutembelea sehemu mbali mbali ikiwemo Hospitali za watu wenye matatizo ya akili, nyumba za waathirika wa madawa ya kulevya.

Akisoma taarifa fupi Mratibu wa mradi wa UNDP ya Ukarabati wa jengo la Tume za Haki za Binaadamu na Utawala Bora Laurant Burilo  amesema jengo hilo limefanyiwa  ukarabati kwa lengo la kuwa na haiba nzuri kwa wafanyakazi .

Alisema ukarabati huo ni pamoja na utiaji wa rangi , uwekaji wa mabango na mageti , utengezaji wa vyoo pamoja na huduma nyengine zote muhimu za kiofisi ambapo jumla yaTsh, Milioni 18 zimetolewa kwa msaada wa UNDP na Denmark.

Kwa upande wake Kamishna wa Tume za Haki za Binaadamu na Utawala Bora Amina Salum Ali  alipokuwan akitambulishwa  aliomba mashirikiano ya pamoja kwa kuwasaidia  wananchi katika kutetea madai ya haki zao  ili kupunguza changamoto .