Asilimia 74 ya wajawazito wanajifungulia kwenye vituo vya Afya

Jumla ya wajawazito 813,923 sawa na asilimia 74 wamejifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma huduma za afya nchini.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa wizara kwa kipindi cha julai hadi desemba 2019 kwa kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya jamii.


“Katika kipindi hiki matarajio yalikua ni wajawazito 1,100,000 wangejifungua,hata hivyo takwimu zinaonesha kuwa jumla ya wajawazito 813,923 sawa na,asilimia 74 walijifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma”Amesema Ummy Mwalimu.

Kwa upande wa wajawazito waliofanya mahudhurio ya kliniki,Waziri huyo amesema kuwa jumla ya wajawazito 797,803 sawa na asilimia 73 ya walengwa walifanya mahudhurio ya kliniki manne na zaidi kama mwongozo ulivyoelekeza.

Aidha, amesema kuwa asilimia 87.4 ya wajawazito sawa na akinamama 886,810 walipatiwa dawa za kukinga Malaria na jumla ya dozi 2,844,174 sawa na asilimia 84.6 walipewa dawa ya kuzuia upungufu wa damu(FEFOL).

Hata hivyo Waziri Ummy amesema,kuwa wizara kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ilihakikisha dawa muhimu za kuzuia na kutibu kifafa cha mimba na kukinga na kutibu kupoteza damu baada ya kujifungua,kutibu magonjwa na,watoto chini ya miaka mitano uliimarika kwa zaidi ya asilimia 85.