https://monetag.com/?ref_id=TTIb Babu Duni: Dhamira yetu Z’bar haijatimia, hatuchoki | Muungwana BLOG

Babu Duni: Dhamira yetu Z’bar haijatimia, hatuchoki

JUMA Duni Haji, mwanasiasa mkongo wa upinzani visiwani Zanzibar amesema, dhamira ya ‘kuwanusuru’ Wazanzibari haijatimia na hawatachoka.

Ametoa kauli hiyo leo tarehe 27 Januari 2020, wakati wa maadhimisho ya miaka 19 ya mauaji ya wanachama wa CUF yaliyotokea tarehe 27 Januari 2001.

“Wakati wa mauaji yale nilikuwa bado kijana, si kama leo nimejaa mvi. Muangalieni Maalim Seif Shariff sote, tunazeekea katika siasa maana dhamira yetu haijatimia.

“Zanzibar inaendelea kutawaliwa kikatili. Uchaguzi uliopo ni kama ule uliolazimisha Afro-Shirazi (ASP) kupindua serikali ya uhuru. Tunataka uchaguzi wa kidemokrasia sio kila uchaguzi watu waumizwe na hata kuuliwa,” ameseba Babu Duni.

Amedai, mauaji ya 2001 yalikusudiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), chini ya uongozi wa Benjamin Mkapa ambaye hajajuta, wala kuomba radhi Wazanzibari na familia ambazo ziliathirika.

Babu Duni ambaye ni Naibu Kiongozi wa Chama cha ACT- Wazalendo, amesema yeye na wenzake wanaongoza chama hicho kwa kufuata Katiba ya nchi na sheria zake.

“Tunaongoza chama cha siasa sio kundi la wahuni au waovu; tunafanya kazi ya kushawishi umma utuamini kuwa hivi tunavozeeka na siasa, tunapigania kutimiza dhamira tuliyonayo ya kuwaletea maendeleo watu na nchi,” amesema na kuongeza:

“Na tunaifanya kazi hii kwa uadilifu na utu wa kiwango cha juu kwa sababu, ndivyo Katiba ya chama chetu inavyoelekeza na Katiba ya nchi inavyohimiza.”

Babu Duni amesema, hataacha mapambano mpaka dhamira yao itimie.

Amedai, baada ya kushindwa uchaguzi 2000, serikali ya Rais Mkapa iliagiza majeshi kuvamia vituo vya uchaguzi na kupora masanduku ya kura, na baadaye kuzichoma moto kura na kuandaa kura bandia zilizowezesha Tume ya Uchaguzi kutangazia ushindi CCM.

“Ule uchaguzi kama ilivyokuwa uliotangulia, tulishinda lakini wakatumia dola kujitangazia ushindi. Tumekuwa tukiendelea kuona uchaguzi wa kutimiza wajibu tu huku wakidanganya dunia…

“Hawataki uchaguzi wa kidemokrasia, ndio maana husema wazi watashinda hata kwa kura moja,” amesema.