Kairuki apongeza uzalishaji wa tofali katika kiwanda cha SHAFA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Uwekezaji Mhe. Angellah Kairuki ametembelea na kukagua mazingira ya uendeshaji wa kiwanda cha vifaa vya ujenzi cha SHAFA na kupongeza uzalishaji wa tofali kiwandani hapo na kusema ni wa kuridhisha.

Ametoa pongezi hizo alipotembelea kiwandani  Januari 20, 2020 ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Pwani ili kukagua mazingira ya wawekezaji,  kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili ili kuendelea kuwa na mazingira mazuri ya wafanya biashara na wawekezaji nchini.

Aidha katika ziara yake aliambatana na Watendaji kutoa Ofisi yake, Uongozi wa Mkoa wa Pwani, Watendaji kutoka Wilaya ya Mkuranga pamoja na watendaji wa Taasisi za Serikali ikiwemo TANESCO, TARURA, TRA, na Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC).

Akizungumza na waandishi wa habari kiwandani hapo, alisema amevutiwa na uwekezaji katika kiwanda hicho kwa kuwa na matofali bora kwa kuzingatia muhimu wa mahitaji ya ujenzi katika kuhakikisha kuna kuwa na majengo bora, kiasa na imara kwa matumizi mbalimbali.

“Vipo viwanda zaidi ya vitatu vinavyotengeneza tofali nchini ingawa hiki kinaongoza kwa kuwa na mitambo ya kisasa aina ya  MASA yenye uwezo wa kuzalisha tofali 10,000, vigae vya sakafuni  zaidi ya 10,000 kwa siku ukilinganisha na viwanda vingine na kwa nchi za Afrika Mashariki ni kiwanda cha mfano kwa kutoa matofali yenye ubora wa hali ya juu,”alesisitiza Waziri Kairuki.

Alieleza kuwa, ipo haja ya kuunga mkono jitihada za wawekezaji wa viwanda kama hivyo ili kuendelea kujieletea maendeleo ya nchi kwa ujumla kwa kuzingatia mchango wake katika ngazi zote kuanzia Kijiji, Taifa hadi nje ya nchi.

Aliongezea kuwa , furaha yake ni kuona kiwanda kinaweza kuzalisha kwa haraka, ubora na idadi kubwa kwa siku ili kuhakikisha kuna kuwa na majengo salama na yenye kudumu hadi vizazi vijavyo.

Akiwasilisha taarifa ya kiwanda kwa waziri, Afisa Mahusiano wa kiwanda hicho Bw. Agrey Roodluck alieleza malengo ya mradi ni pamoja na kuongeza wigo katika sekta ya ujenzi kwa kuzingatia uzalishaji wake unalenga kuwa na aina tofauti tofauti za matofali yenye ubora na kuweza kukidhi mahitaji kwa gharama nafuu.

“Mradi umezingatia changamoto zilizopo za ukosefu wa matofali bora katika maeneo mengi yanayohitajika katika ujenzi wa maegesho ya magari, bararaba, maeneo ya viwanja vya ndege pamoja na majengo makubwa na madogo,”alieleza Roodlucky

Aidha alitoa omba kwa waziri kuendelea kuhamasisha ujenzi salama wa majengo ya taasisi, nyumba ndogo na kubwa kwa kuendelea kutumia tofali za kiwanda hicho na kueleza kuwa ni sehemu ya kuunga mkono maendeleo ya nchi kwa kuzingatia malighafi zinazotumika zinatoka nchini.

“Hadi kukamilika kwa mradi huu utatumia jumla ya Tshs Bilioni 15.3  na tayari zaidi ya asilimia 90 zimeshatumika na asilimia 99.9 za malighafi za kiwanda zinatoka hapa hapa nchini ikiwemo saruji, mchanga, kokoto na maji,”alisisitiza

Sambamba na hilo alisema, lengo kuhakikisha kiwanda kinatoa mchango katika pato la taifa katika kuhakikisha kinalipa kodi zote zinazotakiwa na kuendelea kuzalisha ajira zaidi ya 100 zitakazozingatia kundi kubwa la vijana wazawa ili kuweza kuendesha mitambo iliyopo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Filberto Sanga alimshukuru waziri kwa kutembelea mradi huo, na kueleza kuwa, ni mradi wenye faidi katika Wilaya yake kwa kuzingatia mchango wa mradi na namna walivyojikita katika kuhakikisha wanakuwa wenye bidhaa bora na kukidhi mahitaji ya wateja wake.