https://monetag.com/?ref_id=TTIb Manispaa ya Iringa yapitisha bajeti ya Bilioni 35 | Muungwana BLOG

Manispaa ya Iringa yapitisha bajeti ya Bilioni 35

Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imepitisha bajeti ya sh. Bilioni 35 katika kikao cha baraza kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kimaendeleo kwa mwaka wa fedha wa 2020/2021.
Bajeti hiyo imepitishwa leo katika kikao cha kawaida cha baraza la madiwani cha ambapo kiasi cha sh. Bilioni 24.9 zitatumika kwa ajili ya mishahara ya wafanyakazi wa halmashauri ya manispaa ya Iringa.

Akizungumza kwenye baraza la madiwani kilichoketi jana kwenye ukumbi wa manispaa mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa ya Iringa, Hamid Njovu alisema kuwa kati ya hizo bilioni 5 zitatumika katika miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha wa 2020/2021.

Aidha amesema kuwa mambo ambayo yametekelezwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019 ni pamoja na kukusanya mapato ya ndani kwa asilimia 100.3 hali ambayo kwa kiasi kikubwa imewezesha miradi mbalimbali kutekelezwa kwa asilimia kubwa.

Hata hivyo Mkurugenzi wa manispaa ya Iringa Himid Njovu amesema kuwa bajeti iliyopo watapewa wahusika wakutekeleza majukumu hayo na kuyaishi na kuyasimamia ili mabadiliko yaonekane katika Mkoa wa Iringa.

Alisema kuwa uongozi umeweka utaratibu wa kuandaa maandiko maalumu kwa ajili ya kuombea fedha katika taasisi,mashirika na wadau mbalimbali ili kutekeleza miradi ya umwagiliaji katika skimu ya Kitwiru,Mkoga na uboreshaji wa eneo la utalii la Tungamalenga.

Njovu alilipongeza baraza za madiwani kwa kutekeleza miradi ya mwaka wa fedha wa 2019/2020 kwa kufikia asilimia 136.3 ambapo ilikuwa imevuka lengo ambalo Manispaa walikuwa wamejiwekea katika kukuza uchumi na kuleta maendeleo.

Kwa asilimia kuwa miradi ya mwaka 2019/202 ilitumia bajeti ya mapato ya ndani yanayotokana na makusanyo mbalimbali ya kodi kutoka kwenye vyanzo vyetu vya ndani miradi iliyotekelezwa kuonekana.

Kwa upande wake meya wa manispaa ya Iringa, Alex Kimbe aliwapongeza madiwani kwa kuweza kushirikiana vyema katika kuleta maendeleo ya manispaa kutokana na kupeana ushirikiano katika majukumu ya kila siku ya baraza na vikao mbalimbali vya kamati.

Kimbe alisema kuwa mafanikio yanayoonekana katika manispaa ya Iringa ni ushirikiano mkubwa baina ya madiwani na manispaa hali ambayo imesababisha miradi mingi kuweza kutekelezwa kwa asilimia kubwa na kusema kuwa miradi ambayo haijakamilika inatarajia kukamilishwa kwa bajeti ya msimu wa 2020/2021.

Wakati huo huo aliyekuwa diwani wa kata ya Ilala, Godfrey Mlowe alifikisha barua ya kujiuzulu wadhifa huo na kujivua uanachama wa chama cha Chadema na katika baraza hilo lilofanyika hakuweza kutokea hali ambayo diwani wa kata ya Ruaha Tande Sanga alitumia nafasi ya kutoa hoja kupiga kijembe kwamba wapinzani hawana jipya na kwa kusema mmoja wa madiwani kuona kazi nzuri na kufanya maamuzi kuhamia CCM.