Na Hamisi Abdulrahmani, Masasi
SERIKALI imeshauriwa kuangalia kwa kina utendaji kazi wa wakala ya usambazaji maji na usafi na mazingira vijijini( RUWASA) kwa vile miradi mingi ya maji vijijini wilayani Masasi mkoani Mtwara haitekelezwi kwa ufanisi.
Ushauri huo ulitolewa jana wilayani Masasi na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Masasi,wakati walipokuwa wakichangia hoja za miradi ya maji kwenye kikao cha baraza la madiwani.
Samson Bushiri,diwani kata ya Mpindimbi alisema kumekuwa na harufu ya hujuma katika miradi ya maji vijijini kunakofanywa na jumuhiya za maji vijijini.
Alisema serikali imeanzisha RUWASA kwa lengo la kuboresha huduma za maji hasa kwa wananchi wa vijijini ili waweze kupata maji safi na salama.
Bushiri alisema katika miradi ya maji wa Mpindimbi zaidi ya sh.milioni 19 zinaonekana kuhujumiwa na jumuhiya ya maji hivyo kuzorotesha huduma ya maji kwa wananchi.
Edward Mahelela diwani kata ya Chikolopora, alisema RUWASA iongeze nguvu ya utekelezaji wa miradi ya maji vijijini ili wananchi waweze kupata huduma ya maji bila ya kikwazo.
Naye mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Masasi,Juma Satma alisema wanaishauri serikali kuangalia utendaji kazi wa utekelezaji wa miradi ya maji vijijini.
Alisema miradi mingi ya maji vijijini tangu ilivyotoka chini ya halmashauri na kuwa chini ya RUWASA imepoteza hadhi yake na kuzorotesha huduma ya maji kwa wananchi.jumuhiya ya maji.
Satma alisema wao kama madiwani kutokana na hali hiyo ya miradi ya maji wanaishauri serikali kuangalia uwezekano wa kusimamia vizuri miradi ya maji kupitia RUWASA.
Kwa upande wake,kaimu Injinia wa RUWASA halmashauri ya wilaya ya Masasi,Edger Lyapembile alisema wanatambua changomoto hiyo na wahaifanyia kazi ili miradi ya maji iweze kuwa ya ufanisi.
"Tunatambua sana changamoto za miradi ya maji pamoja na jumuhiya zake za maji na kwamba zipo sheria mbalimbali za maji zimebadilika...tunaahidi tutafanya kazi kwa ufanisi," alisema Lyapembile
Alisema changamoto kubwa iliyojitokeza katika miradi ya maji ni mabadiliko yaliyofanyika ya miradi ya maji kutoka halmashauri na kuundwa kwa RUWASA ambapo mikataba nayo ilipaswa kubadilisha.
Lyapembile alisema hapo ndipo ilisababisha kucheleshwa kwa utekelezaji wa miradi mingi ya maji lakini hivi sasa kila kitu kitakuwa sawa.