Waziri Kairuki azindua kongamano na mwongozo wa uwekezaji Songwe

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji Angella Kairuki mapema leo amezindua Kongamano na Mwongozo wa Uwekezaji Mkoa wa Songwe huku akiwahakikishia washiriki wa Kongamano hilo kuwa Mkoa wa Songwe ni mahali salama kwa uwekezeji.

Waziri Kairuki amesema Songwe ina fursa za uwekezaji na biashara ndani ya Mkoa lakini pia ina nafasi kipekee ya Kimkakati iliyonayo kwakuwa ni Lango Kuu la SADC na hivyo kuwa kiungo cha kibicashara kati ya Tanzania na Nchi 6 kati ya 16 za SADC.

“Ni matumaini yangu kuwa kaulimbiu ya Songwe Lango la SADC  itaenda sambamba na kuhamasisha biashara kati ya Mkoa wa Songwe na Mikoa ya jirani, lakini pia biashara baina ya Mikoa ya jirani na Nchi za SADC kupitia Mkoa huu wa Songwe, Wekeni mikakati mizuri ya kufanikisha hili.”, amesisitiza Waziri Kairuki.


Ameongeza kuwa Mwongozo wa Uwekezaji aliouzinduaumebainisha kwa undani fursa nyingi za uwekezaji  zilizopo Mkoa wa Songwe ikiwa ni pamoja na Kilimo, Mifugo, madini, utalii na uhifadhi wa Misitu, na kuwa  fursa zote hizi zinaufanya Songwe kuwa eneo zuri la kuvutia wawekezaji.

Waziri Kairuki ametumia nafasi hiyo pia kukumbushia maagizo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mikoa ambayo bado haijaandaa Mwongozo wa Uwekezaji kufanye hivyo mapema huku akiupongeza uongozi wa Mkoa wa Songwe kwa kuwapokea vizuri wawekezaji kwakuwa hajawahi kupokea malalamiko yoyote kutoka kwa wawekezaji.

Pia ametoa rai kwa Halmashauri zote nchini kukamilisha mchakato wa kutenga ardhi katika maeneo yao kwa ajili ya uwekezaji na kuyawekea miundombinu stahiki ya msingi huku akielezea kuwa eneo linaweza kuwa dogo ila lenye miundombinu ya kuvutia wawekezaji.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela amesema Mkoa wa Songwe unazo sifa nyingi za kuwavutia wawekezaji ikiwa ni pamoja na halmashauri zote tano kutenga maeneo ya Uwekezaji.

Brig. Jen. Mwangela amesema Mkoa wa Songwe unavutia wawekezaji katika kilimo cha kisasa cha Umwagiliaji kwakuwa hali ya hewa inaruhusu na kuna eneo la hekta 18,464 linalo faa kwa kilimo cha Mbogamboga na matunda huku kukiwa na miundombinu ya barabara na usafiri wa anga ili kuwezesha kusafirisha bidhaa hizo katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Amezitaja fursa nyingine ni uwekezaji katika Kilimo cha Mbegu, Usambazaji wa pembejeo na Zana za Kilimo, fursa ya mitambo ya kukaushia mazao, fursa ya kuanzisha Ranchi, fursa ya mashamba ya kutotoleshea vifaranga, fursa katika utalii kwenye maeneo ya utalii wa  uwindaji, fursa ya makampuni ya kuongoza watalii na kujenga hoteli za kitalii na Campsites.

Brig. Jen. Mwangela amesema matarajio ya Mkoa ni kuwa baada ya Kongamano hilo wawekezaji watapatikana katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Songwe David Kafulila amesema Takwimu za Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) zinaonyesha kuwa alisilimia 70 ya mizigo inayotoka bandari ya Dar Es Salaam kuelekea nchi za SADC huzifikia nchi hizo hupitia mpaka wa Tunduma uliopo Mkoani Songwe.

Kafulila amefafanua kuwa hiyo ni fursa kubwa kwa wawekezaji kwani wanaweza kujenga maeneo ya kutunzia bidhaa, maegesho, bandari kavu na bandari huru katika Mkoa wa Songwe ambapo kwa sasa fursa hizo bado hazija tumiwa vizuri.

Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Shanta Gold Mine Roman Urasa amesema fursa ambayo Mkoa wa Songwe ya kuwa Lango la SADC isiishie  kuwa njia tu ya bidhaa kwenda ya nchi jirani bali  Songwe izalishe bidhaa za kusafirisha nje ya nchi.