Mpinzani mkuu wa Netanyahu achaguliwa kuwa spika wa Israel


Mpinzani mkuu wa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, Benny Gantz amechaguliwa jana kuwa spika wa bunge, hatua ambayo haikutarajiwa na ambayo huenda ikatoa fursa ya kufikiwa mpango wa kugawana madaraka kati ya watu hao wawili wakati nchi hiyo ikipambana na mgogoro wa virusi vya corona.

Kurejea kwa Gantz, ambaye alimaliza mwaka uliopita akijaribu kumuondoa madarakani Netanyahu katika chaguzi tatu zenye kinyang'anyiro kikali ambazo hazikumpata mshindi wa moja kwa moja, anaonekana kumpa waziri mkuu huyo fursa nyingine maishani, wakati akijiandaa kufika mahakamani kwa mashitaka ya ufisadi.

Pia imezusha shutuma kali kutoka kwa washirika wake wa kisiasa ambao wanamtuhumu kwa usaliti, na kukigawa chama chake cha Bluu na Nyeupe, ambacho ni muungano wa makundi matatu yanayompinga Netanyahu.