https://monetag.com/?ref_id=TTIb Polisi aliyetoa wazo kuanzishwa kituo cha huduma ya pamoja apandishwa cheo | Muungwana BLOG

Polisi aliyetoa wazo kuanzishwa kituo cha huduma ya pamoja apandishwa cheo


Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) nchini Tanzania, Simon Sirro amempandisha cheo Christina Onyango kuwa mkaguzi msaidizi wa Polisi. Awali Christina alikuwa konstebo.

Hivi karibuni Christina alitunukiwa shahada ya udaktari katika Chuo Kikuu cha Lead Impact kilichopo Marekani kutokana na utendaji wake.

Askari huyo alitoa wazo la kuanzishwa kituo cha huduma ya pamoja kati ya Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam na taasisi nyingine za Serikali zinazojishughulisha na masuala ya kupinga ukatili wa kijinsia ambacho kipo katika Hospitali ya rufaa ya Amana manispaa ya Ilala, jijini Dar es Salaam.

Machi 11, 2020, IGP Sirro alimpongeza kwa barua na kumpandisha cheo kuwa mkaguzi msaidizi wa polisi na kumuelekeza Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa kumvalisha cheo kipya.

Leo Alhamisi Machi 26, 2020, Kamanda Mambosasa amemvalisha cheo Christina na kumpongeza kwa kuliwakilisha jeshi hilo vizuri katika jamii.