Na John Walter, Babati
Chama cha wafanyakazi wa serikali za mitaa Tanzania [TALGWU] Mkoa kimetoa mafunzo kwa watumishi wa kada ya afya katika hospitali ya Dareda iliyopo Wilaya ya Babati ili waweze kujikinga na virusi vya COVID-19 wakati wanatoa huduma kwa wagonjwa.
Katibu wa chama cha wafanyakazi wa serikali za mitaa Mkoa wa Manyara Ndulilah Pandauyaga akizungumza leo machi 26 katika mafunzo hayo, amesema kuwa chama hicho kimeamua kutoa elimu hiyo kwa watumishi wa afya kutokana na chama hicho kuwa na wanachama wengi kutoka idara ya afya hivyo endapo itatokea mlipuko wa ugonjwa huo kwa wataalamu hao chama hicho kinaweza kupoteza wanachama wengi.
Amesema kuwa wauguzi wakijilinda wakiwa na afya nzuri wananchi wanakuwa na matumaini makubwa ya kutibiwa kwa uhakika hivyo kutolewa kwa elimu hiyo itawasaidia .
Naye katibu wa afya wilaya ya Babati Suten Mwambulambo alisema kuwa ni vyema Wataalamu wa afya kujikinga wao na familia zao na ugonjwa wa corona na kuacha tabia ya kujitenga kwani wao pia ni binadamu na kwamba wanaweza kuathiriwa na ugonjwa huo bila kujali taaluma zao.
Joseph Lorri ni Mganga mkuu wa hospitali ya Dareda anaeleza kuwa mafunzo hayo yamewafanya wazidi kuwa makini katika kutoa huduma kwa umakini mkubwa na kujikinga na maambukizi dhidiya Corona.
Mafunzo hayo yalijumuisha watumishi wote wa hospitali ya Dareda,Wauguzi,Madaktari,Walinzi ,Mafundi pamoja na wafanya usafi.
Aidha alieleza kuwa barakoa na vitakasa mikono vimekuwa ni adimu kupatikana kwa sasa lakini awali kabla ya ugonjwa huu kuingia hapa nchini walikuwa nazo nyingi na zilikuwa zikitumika kwenye upasuaji na watu wanaofanya usafi nje, baada ya ugonjwa kuingia ikaonekana kila mtumishi anataka kuvaa ndio shida ikatokea na katika muda mfupi tukaishiwa
‘’Tumejaribu kutafta wale wanaosambazia hivi vifaa wanasema hazipatikani, na hatujui tunaenda kuzipatia wapi na hata wakati mwingine ukizipata unakuta bei inaongezeka siyo sawa na zamani walivyokuwa wakiuza’’ alisema.
Hata hivyo mganga mfawidhi wilaya ya Babati Madama Hosea alikiri ni kweli kumekuwa na upungufu wa dawa ikiwa ni pamoja na vitakasa mikono na hivyo wanafanya mawasiliano na Bohari kuu ya madawa kwa ajili kupatiwa madawa na vifaa hivyo baada ya muda mfupi vitaletwa kwani tayari wameshaomba.