Jeshi la polisi Mkoa kaskazini Pemba lajipanga kuwafutia leseni madereva wazembe

JESHI la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba linajipanga kuiandikia barua wizara ya mawasiliano ili kuomba wafutiwe leseni madereva wazembe wanaosababisha vifo.

Kauli ilitolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa huo , Kamishna Msaidizi Mwandamizi Juma Sadi Khamis wakati akizungumza kufuatia kutokea ajali iliyosababisha kifo cha mtu mmoja na wengine watatu kujeruhiwa.

Alisema jeshi la Polisi limekuwa likitoa taaluma kwa madereva kuheshimu sheria za usalama  barabarani, lengo ni kuwataka kufuata sheria ili kunusuru maisha ya abiria wasio na hatia.

“Tumeona njia sahihi ya kukabiliana na ajali ni kuwafutia leseni madereva  wazembe wanaosababisha vifo na ulemavu kwa baadhi ya wananchi”alieleza.

Hivyo Kamanda wa Sadi aliwataka madereva kusimamia na kufauata sheria bila ya kushurtishwa lengo ni kulinda uhai  na maisha ya watu.

Kamanda Sadi aliyasema hayo baada ya gari ya mizigo aina ya HINO yenye namba za usaliji Z 301 HJ iliyokuwa ikiendeshwa na dereva Amour Saleh Seif kuacha njia na kupinduka na kusabisha kifo cha mtu mmoja mkaazi wa Micheweni Pemba.

Aliyefariki kutokana na ajali hiyo ni Mahadi Subeti Khamis 20 ambapo waliojeruhiwa na kulazwa hospitali ya Micheweni ni Ali Dawa Faki 18, Faki Dawa Faki 32 na Ali Suleiman Ali 34.

Kamanda wa polisi mkoa wa Kaskazini Pemba kamishna Msaidizi Mwandamizi Juma Sadi Khamis alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi.

Kamanda Sadi alisema ajali hiyo ilitokea mei 28 majira ya saa tatu na robo , ambapo dereva huyo gari ilimshinda na kuacha njia na kupinduka.

“Uchunguzi wa awali ilibaini kwamba chanzo cha ajali hio ni mwendo kasi kwani dereva ilimshinda gari na kuacha njia na kupinduka na hivyo kusababisha kifo hicho na majeruhi watatu”alisema.

Kamanda sadi alitoa wito kwa madereva kufuata sheria ya usalama barabarani ili kuepusha ajali ambazo zinaweza kuepukika.