Maandamano ya Mei Mosi ulimwenguni yaathiriwa na corona


Wafanyakazi mjini Hong Kong waliojaribu kuandamana kama ilivyo desturi ya siku ya kimataifa ya wafanyakazi, Mei Mosi, wamezuiliwa kuandamana kufuatia maambukizo ya virusi vya corona.

 Hata hivyo baadhi yao waliovalia barakoa walielekea mitaani huku wengine wakielezea hisia zao kupitia mitandao ya kijamii.

Kwa kawaida mamilioni ya wafanyakazi hujitokeza mitaani kuandamana siku hii ya kimataifa ya wafanyakazi.

 Lakini kufuatia masharti ya watu kukaa mbalimbali, utamaduni huo uliozoleka haujashuhudiwa leo katika miji mingi.

Nchini Ufaransa, ambayo bado iko chini ya amri ya kutosafiri, wafanyakazi wanaiadhimisha siku yao kupitia mitandao ya kijamii au kwenye mabaraza ya nyumba zao.

Mjini Berlin Ujerumani, takriban maafisa 5,000 watakuwa wakifanya doria mitaani kukabiliana na watakaokiuka maagizo ya watu kukaa mbalimbali endapo wafanyakazi wataandamana.