https://monetag.com/?ref_id=TTIb Ukatili wa polisi wa Marekani dhidi ya Wamarekani weusi, wasababisha kifo cha mtu mwingine | Muungwana BLOG

Ukatili wa polisi wa Marekani dhidi ya Wamarekani weusi, wasababisha kifo cha mtu mwingine



Vitendo vya ukatili wa kutisha vya polisi ya Marekani kwa mara nyingine vimepelekea kufariki dunia Mmarekani mweusi.

Jumatatu iliyopita, polisi mweupe nchini Marekani alimuua kikatili Mmarekani mwenye asili ya Afrika katika mji wa Minneapolis, jimbo la Minnesota. Video iliyosambaa kwenye mitandao ya kijamii nchini Marekani, ilimuonyesha polisi mzungu akiwa amemlaza chini mtu huyo kifudifudi huku akiwa amemkandamiza vibaya shingo lake kwa goti la mguu wa kushoto.

 Mtu huyo mwenye asili ya Afrika aliyejulikana kwa jina la George Floyd alikuwa akipiga kelele kwa kusema: "Umenibana shingo siwezi kupumua" "Naomba maji" na "Usiniue" hadi alipofariki dunia. Kufuatia ukatili huo wa kutisha, meya wa mji wa Minneapolis, Jacob Frey amewafuta kazi maafisa wanne wa polisi kwa kusababisha kifo cha Floyd.


Vitendo vya ukatili wa polisi wa Marekani dhidi ya Wamarekani weusi, vimekuwa vikiibua maandamano na malalamiko ya raia wa nchi hiyo. Mauaji dhidi ya Wamarekani weusi nchini humo yanayofanywa na polisi yalishika kasi kuanzia mwaka 2014 suala ambalo limeibua harakati za kiraia pamoja na vitendo vya utumiaji mabavu na hata machafuko ya siku kadhaa katika majimbo kadhaa ya nchi hiyo. Kwa kawaida mahakama za Marekani huwa zinawaachilia huru polisi wanaotenda jinai dhidi ya Wamarekani weusi au kuwapa adhabu hafifu ikilinganishwa na makosa waliyofanya.