Fauci aonya Marekani imepata pigo baya la corona


Merekani inapambana kudhibiti ongezeko la maambukizi ya virusi vya korona katika majimbo yake kadhaa. Umoja wa Ulaya kwa upande wake unatafakari iwapo utawaruhusu wasafiri wa Marekani kuingia katika mataifa yake.

Marekani inakabiliwa na kipindi kigumu, wakati Umoja wa Ulaya Jumanne ukitishia kuwazuia raia wa nchi hiyo kuingia kwenye mataifa yake, kutokana na kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya korona katika majimbo tofauti ya Marekani.

Daktari mkuu nchini Marekani, Anthony Fauci, amekiri kwamba Marekani imepata pigo baya sana, huku maambukizi katika majimbo ya Florida, Arizona na Texas yakizindi kuongezeka idadi. Amesema ana wasiwasi mkubwa, na kwamba wiki chache zijazo zitakuwa muhimu kuonyesha uwezo wa Marekani katika kupambana na maambukizi hayo.

Soma zaidi:Maambukizi ya COVID-19 bado yaongezeka duniani

Fauci na maafisa wengine wa afya wamesema hawakupewa agizo la kupunguza vipimo vya ugonjwa wa COVID-19, kufuatia matamshi ya Rais Donald Trump ya kufanya vipimo vichache kutokna na kwamba majibu mengi yanathibitisha kuwepo kwa ugonjwa huo. Fauci amesisitiza kwamba wataendelea kufanya vipimo hivyo, wakati akizungumza na kamati ya araza la wawakilishi la Marekani.

Fauci pia aliwasihi raia kujiepusha na mikusanyiko mikubwa na kuvaa barakoa wakati wakiwa karibu na watu wengine kujaribu kuzuia kuongezeka kwa maambukizi hayo, wakati Trump akiendelea kupuuza ushauri wa namna hiyo, na kufanya mikutano ya hadhara.


Wakati huo huo, nchi kadhaa za Umoja wa Ulaya zimeelezea wasiwasi juu ya kufungua mipaka yake kwa raia wa Marekani, kwani wanautilia shaka usimamizi wa Rais Donald Trump wa janga hilo la virusi vya korona.

Marekani inayotajwa kuwa na idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya korona duniani kote, inashuhudia ongezeko la maambukizi mapya ya ugonjwa huo wa COVID-19. Wasafiri wa Marekani huenda watawekwa kundi moja na wasafiri wa Brazil na Urusi ambao wako nafasi ya pili na ya tatu ulimwenguni kwa kuwa na idadi kubwa ya maambukizi nchini mwao.

Mwanzoni mwa mwezi Machi, wakati idadi ya maambukizi ilivyokuwa ikiongezeka barani Ulaya, Trump aliwawekea marufuku raia wa Ulaya kuingia nchini Marekani. Umoja wa Ulaya, unaweza kutangaza wiki ijayo mwendelezo wa marufuku kwa Wamarekani kuingia katika nchi zake, wakati mipaka inatarajiwa kufunguliwa kwa wasafiri kutoka nje ya umoja huo mnamo Julai 1.

Zaidi ya watu milioni 27 nchini Marekani wameshafanyiwa vipimo vya virusi vya korona, na milioni 2.3 miongoni mwao wamekutikana na virusi hivyo. Aidha vifo zaidi ya 120,000 vimesharikodiwa nchini humo vinavyohusishwa na ugonjwa wa COVID-19.