Chama cha UDP chatangaza kumuunga mkono mgombea wa CCM


Chama cha United Democratic Party (UDP) kimetangaza rasmi kumuunga mkono mgombea wa Urais kupitia CCM, Dkt. John Magufuli kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2020.

Maamuzi hayo yametangazwa na Mwenyekiti wa chama hicho, John Cheyo Jijini Dar es Salaam leo, ambapo amesema wameamua kufanya hivyo kutokana na kuridhishwa na utendaji kazi wake katika kipindi cha miaka mitano.

"Kwa upande wa Rais, UDP inasema endapo CCM watamchagua John Pombe Magufuli, tutamfanyia kampeni kwa sababu amefanya mambo mazuri. Kitu ninachojivunia ni kwamba amefanya Watanzania tujiamini", amesema Cheyo.

"Miaka yangu yote 15 nipo Bungeni nilikuwa naipigia kura bajeti, wengine wanaitana pembeni waseme hapana. Sasa unaposema hapana na mshahara wako utasema hapana?, baada ya hapo unawaona dirishani wanaomba hela zitoke wapi?", ameongeza.

Amesema kuwa chama hicho kinapigania maslahi ya wakulima nchini na kuwataka Wabunge na Madiwani kupigania kufa na kupona kwa ajili ya wakulima hao.