Hatimaye Trump avaa barakoa


Rais wa Marekani Donald Trump amevaa barakoa kwa mara ya kwanza hadharani tangu lilipoanza janga la virusi vya corona.`
Rais huyo amevaa barakoa alipotembelea hospitali ya kijeshi ya Walter Reed iliyopo nje ya jiji la Washington, ambako alikutana na wanajeshi waliojeruhiwa na wahudumu wa afya.
"Sijawahi kamwe kupinga uvaaji wa barakoa, lakini ninaamini kuwa zina mahali na muda wake," alisema alipokuwa akiondoka katika ikulu ya White House.
Awali alisema kuwa hawezi kuvaa barakoa na akamkejeli hasimu wake wa chama cha Democrat Joe Biden kwa kufanya hivyo.
Lakini Jumamosi alisema kuwa : "Ninafikiri pale unapokua hospitali, hasa katika hali fulani, ambapo unaongea na wanajeshi na watu, ambao wakati fulani wametoka kwenye meza za upasuaji, nafikiri ni kitu kizuri kuvaa barakoa ."
Akizungumza na kituo cha habari za biashara cha - Fox Business Network wiki iliyopita Bwana Trump alisema : "Ninaunga mkono barakoa."
Aliongeza kuwa "ni kama ninapenda " anavyofanana akiwa ameivaa, akijifananisha na aliyovaa Lone Ranger, shujaa wa kufikirika ambaye pamoja na rafiki yake mzawa wa Marekani, Toronto, walipigana na wahalifu katika Marekani ya zamani ya Magharibi.
Lakini wakati vituo vya Marekani vya udhibiti wa magonjwa (CDC) mwezi Aprili vilipopendekeza kuwa watu wavae barakoa au vitambaa vinavyofunika midomo na pua wawapo katika maeneo ya umma ili kusaidia kuzuwia kusambaa kwa virusi, Bwana Trump aliwaambia waandishi wa habari kuwa hatafuata agizo hilo.
"Sidhani nitakua nikifanya hilo" alisema wakati huo. " Kuvaa barakoa huku nikiwasalimia marais, mawaziri wakuu, madikteta, wafalme na mamalkia -sioni hili likifanyika."
Baadhi ya taarifa za vyombo vya habari zimesema kuwa washirika wake wamekua wakimuomba mara kwa mara rais Trump avae barakoa awapo hadharani.

arekani imeshuhudia maambukizi mapya ya watu 66,528 katika kipindi cha saa 24 zilizopita, rekodi ya siku moja, na jumla ya takriban vifo 135,000 tangu janga la virusi vya corona lilipoanza, kulingana na data za Chuo Kikuu cha Johns Hopkins.
Louisiana ni jimbo la hivi karibuni lililoagiza watu wavae barakoa katika maeneo ya umma.
Gavana kutoka chama cha Democratic John Bel Edwards pia ameagiza kufungwa kwa baa kote Louisiana, na kuweka sheria kalio kuhusu uendeshwaji wa migahawa ya chakula, ambayo haitaweza kuwahudumia wateja ndani yake. Hatua hizozitaanza kutekelezwa kuanzia Jumatatu.
Wabunge wa Republican wanatarajiwa kupinga hatua hiyo.