https://monetag.com/?ref_id=TTIb Jinsi ya kujikinga na vidonda vya tumbo | Muungwana BLOG

Jinsi ya kujikinga na vidonda vya tumbo

Nini husababisha vidonda vya tumbo?
Kisababishi kikuu ni bakteria aina ya helicobacter pylori ni kupitia vyakula na maji. Pia, hupatikana kwenye mate ya binadamu hivyo inaweza kusambazwa mdomo kwa mdomo kama wapenzi wanaonyonyana ndimi.

Bakteria hao huishi kwenye kuta za utumbo na hutengeneza vimeng’enya viitwayo urease inayopunguza athari za asidi kwenye utumbo.

Utumbo hutaka kufidia kiasi cha asidi kinachopotea kwa kutengeneza zaidi na husababisha kukwangua kuta za utumbo.

Sababu nyingine ni chembe za urithi genetics. Idadi kubwa ya watu wenye vidonda vya tumbo wana ndugu wa karibu na wenye vidonda pia. Hii huwafanya wataalamu kufikiria kuwa chembe za urithi zinahusika pia.

Uvutaji sigara na tumbaku. Wavutaji wa sigara wako katika hatari ya kupata vidonda vya tumbo ikilinganishwa na wasiovuta. Matumizi ya pombe/vilevi. Walevi wako katika hatari zaidi ya kupata vidonda vya tumbo ikilinganishwa na wasiotumia vileo.

Msongo wa mawazo. Msongo wa mawazo hausababishi vidonda moja kwa moja ila hufanya hali kuwa mbaya zaidi kwa wagonjwa.

Dalili za vidonda
Ieleweke ni mara chache mtu kuugua vidonda vya tumbo na kutoonyesha dalili.

Zifuatazo ni dalili zinazotokea kwa wagojwa wengi;
Maumivu ya tumbo na huwa makali zaidi pale asidi inapopita juu ya vidonda.
Maumivu yanaweza kuanzia kwenye kitovu na kupanda juu hadi katikati ya kifua.
Maumivu yanaweza kuongezeka unapokuwa njaa. Pia, yanaweza kuwa makali wakati wa usiku yanayoweza kupunguzwa kwa kula chakula kidogo.


Dalili nyingine ni kushindwa kumeza vizuri chakula au kukwama kama kinataka kurudi mdomoni, kujisikia vibaya baada ya kula, kupungua uzito, kukosa hamu ya kula.

Dalili hatari ni pamoja na kutapika damu, kupata choo kikubwa cheusi au chenye damu nzito na kupata kichefuchefu na kutapika.

Jinsi ya kugundua vidonda vya tumbo
Maelezo ya mgonjwa kuhusu dalili humsaidia daktari kuhisi kinachomsumbua mgonjwa kuwa ni vidonda vya tumbo.

Ili kuthibitisha vidonda vipimo vifuatavyo hufanyika. Kupima damu kuangalia bakteria aina ya h.pylori na kama mgonjwa amekuwa akitumia antibayotiki au dawa za vidonda Proton Pump Inhibitors ‘PPIs’ mfano Omeprazole. Vipimo vyake vya damu vitaonyesha majibu hasi.

Kupima pumzi. Mgonjwa hupewa anywe maji yenye atomi za kaboni zinazoweza kuvunjika, hii hufanya bakteria H.pylori kuvunjika na baada ya saa moja mgonjwa hutoa pumzi kwenye chombo kilichofunikwa. Ikiwa mgonjwa ameambukizwa sampuli ya pumzi itaonyesha vipande vya kaboni kwenye kabonidioksaidi.

Kupima antijeni kwenye kinyesi. Kipimo hiki huangalia kama kuna bakteria h.pylori kwenye kinyesi. Vilevile kipimo hiki hutumika kuangalia ufanisi wa matibabu yaliyotolewa dhidi ya bakteria.

Kufanya x-ray ya sehemu ya juu ya tumbo ‘upper gastrointestinal x-ray’. Picha huonyesha ‘esophagus’, mfuko wa tumbo ‘stomach’ na dudenum. Mgonjwa humeza maji yenye ‘Barium’ ambayo hufanya vidonda kuonekana kirahisi kwenye x-ray.

Matibabu
Kama vidonda vitakuwa vimesababishwa na bakteria h.pylori dawa za kuua na kuondoa bakteria hutumiwa.

Kama vidonda vya tumbo vitakuwa vimesababishwa na ‘NSAIDs’ na hana maambukizi ya bakteria h.pylori atapaswa kutumia dawa Proton Pump Inhibitors ‘PPIs’ mfano Omeprazole, Esomeprazole & Lansoprazole.

Proton Pump Inhibitors ‘PPIs’ hufanya kazi kwa kuvunja/kuzuia kazi ya protini ziitwazo ‘Proton Pump’ ambazo huhusika katika utengenezaji wa asidi tumboni.

Matumizi ya NSAIDs kwa ajili ya kuondoa homa na maumivu yatarithiwa na dawa kama Paracetamol.

Vilevile dawa aina ya H2-Receptor Antagonists mfano Cimetidine, hutumika kama mbadala kama dawa aina ya ‘PPIs’ hazitokuwepo.

H2-Receptor Antagonists hufanya kazi ya kuzuiia utendaji wa protini iitwayo ‘Histamine’ ambayo inahusika na kuchochea utengenezaji wa asidi tumboni.

Matibabu yaliyozungumziwa hapo juu yanaweza kuchukua muda kabla ya kuanza kufanya kazi, hivyo daktari anaweza kuongeza matibabu mengine kama vizuia asidi ‘Antiacids’ & ‘Alginates’ kwa ajili ya nafuu ya haraka.

Namna ya kuishi na vidonda vya tumbo
Mambo yafuatayo yatakusaidia kuishi vizuri ukiwa na vidonda vya tumbo;kuacha kutumia kahawa na chai, kwani vitu hivi huongeza kiwango cha asidi kinachotengenezwa na tumbo lako. Unaweza kutumia chai ya mitishamba kama mbadala.

Kunywa maziwa na vitu vitokanavyo na maziwa kama maziwa mgando na jibini.

Maziwa hufikiriwa kufunika utumbo na kupunguza athari za asidi ya tumboni. Jitahidi kupunguza uzito hasa ikiwa uzito umezidi na hauendani na kimo chako.

Kula angalau kidogo mara kwa mara. Hii itasaidia kupunguza athari za asidi inayotengenezwa na tumbo.

Acha au kunywa vileo siku maalumu tu kwa maana unywaji wa pombe mara kwa mara hutonesha kwenye vidonda vya tumbo vinavyotaka kupona.

Epuka matumizi ya viungo vya vyakula kwa maana hufanya hali kuwa mbaya zaidi.


Acha kuvuta sigara, tumbaku, na bangi. Uvutaji wa sigara utakuweka kwenye hatari zaidi ya kuanza vidonda vipya na kuzuia vidonda vingine visipone.