Kocha Mpya wa Simba Kutua na Kifaa Chake



BAADA ya Kocha wa AS Vita, Frolent Ibenge kuwaita Simba mezani kwa mazungumzo ya kujiunga Simba, huenda kocha huyo akaambatana na kiungo wa timu yake, Jeremy Mumbere ambaye amesema kuwa yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha usajili wa kujiunga na wababe hao wa Msimbazi.

Jeremy Mumbere amekuwa sehemu ya kikosi cha kwanza cha Kocha Frolent Ibenge ndani ya AS Vita ambao wanaweza kukutana kwa pamoja ndani ya Simba itayoshiriki katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao.

Simba imehusishwa kutaka kumshusha kocha Ibenge ili achukue nafasi ya kocha wa sasa, Mbelgiji Sven Vandenbroeck ambaye inadaiwa anaweza kuondoka baada ya msimu kuisha.

Ofisa Habari na Mawasiliano wa Simba, Haji Manara, amekuwa akikaririwa akisema timu hiyo itafanya usajili wa wachezaji wa maana ili kuhahikikisha inafanya vizuri katika michuano ya kimataifa msimu ujao.

Akizungumza Mumbere alithibitisha kuwa katika mazungumzo na Simba huku akiweka wazi kuwa muda si mrefu watamalizana kwa kuwa wapo katika hatua za mwisho za kukamilisha usajili.

“Nipo kwenye mazungumzo ya muda mrefu na Simba, tumefikia sehemu nzuri, lakini bado hatujamalizana, natarajia kuona usajili wangu ukikamilika siku za hivi karibuni baada ya ligi ya Tanzania kumalizika.

“Kuhusu kocha wangu Ibenge kutakiwa na Simba nimesikia tetesi tu zikisema hivyo lakini bado hakuna taarifa kamili kuhusu yeye kujiunga na Simba, ninachokifahamu kuhusu yeye bado ni mwalimu wa AS Vita,” alisema Mumbere.