JKT yaonyesha bidhaa zake kwenye maonyesho ya nanenane Simiyu

JESHI la Kujenga Taifa (JKT) lipo katika Maonesho ya Nanenane ambapo linaonesha bidhaa zake mbalimbali.
 
Akizungumza katika Maonesho ya 27 Nanenane Kitaifa yanayofanyika Nyakabindi mkoani hapa, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Nanenane  Kitaifa  wa jeshi hilo Luteni Kanali Peter Lushika alisema wameshiriki maonesho hayo lengo kubwa likiwa ni kuonesha bidhaa mbalimbali wanazozizalisha kupitia vijana wao.
 
Alisema jeshi hilo limepeleka bidhaa mbalimbali za kilimo, viwanda na  mifugo kwenye maonesho hayo.
 
” Pamoja na kuwepo kwa bidhaa hizo na kuzingatia maendeleo makubwa ya kilimo na uvuvi jeshi letu tumeleta kampuni ya ulinzi kwa ajili ya kulinda wakulima, wafugaji na wavuvi pale wanapo kuwa na kipato baada ya mauzo” alisema Lushika.
 
Alisema katika maonesho hayo jeshi hilo limekuja na shamba darasa ambalo lina mazao mbalimbali zaidi ya aina 20 na lengo likiwa ni kuwafundisha wakulima namna bora ya kilimo cha kisasa kwa kutumia zana walizonazo kama matrekta na virutubisho vingi vya kutosha kwa mfano matumizi ya mbolea hasa za mboji.
 
Alisema jeshi hilo limejikita kwenye mazao ya kimkakati kama zao la pamba ambalo linalimwa zaidi katika mikoa ya Simiyu, Shinyanga na Mara ambalo ni chanzo kikubwa cha malighafi kwenye viwanda vyetu.
 
Alitaja teknolojia nyingine waliyokuja nayo ni ufugaji wa samaki ambapo wanatumia mbinu mpya ya kutotolesha vifaranga aina ya sato na vifaranga aina ya kambale.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti wa Shirika  la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) Meja Peter Sabyiga alisema wanazalisha bidhaa mbalimbali zinazotokana na mazao ya kilimo, mbogamboga na upikaji wa vyakula.
 
Alisema mambo mapya waliokuja nayo kwenye maonesho hayo kama kauli mbiu inavyo sema ya kwa maendeleo ya kilimo na uvuvi chagua viongozi bora 2020  ukifika kwenye banda la JKT utakuta kiwanda cha kutengeneza samani ambacho kinatumia miti  ambayo inazalishwa  kutokana na kilimo cha miti, kiwanda cha maji, kiwanda cha kuzalisha viatu na kuwa malighafi yote hayo yanatokana na mazao ya kilimo kama ufugaji wa mifugo kama ng’ombe na mbuzi ambapo ngozi zao hutumika kutengenezea viatu.
 
Aidha alisema Makamu wa Rais Mama Samia Hassan Suluhu alipotembelea banda lao alihimiza kilimo cha mboga mboga ambacho wamekuwa wakikifanya kwa msaada wa ushauri wa  shirika la TAHA ambalo linasimamia kilimo cha mbogamboga na masoko ya ndani na nje ya nchi.
 
“Tunawaomba wananchi wafike kwenye banda letu waweze kujifunza mbinu za kuzalisha mazao hayo.
 
Afisa Tawala wa Banda la  JKT, Capten Edward Geza  alisema majukumu yake ni kuhakikisha kila kitu kina kwenda sawa na kufanya mawasiliano baina yao na ofisi ya mkuu wa mkoa wa Simiyu kuhusu viongozi na wageni wanaofika kwenye maonesho hayo kwani ni lazima wafikie kwenye jengo la watu maalumu (VIP) ambalo linamilikiwa na jeshi hilo.

Post a Comment

0 Comments