https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mwanaume afariki 'kufuatia kipigo cha polisi' kwa kukiuka masharti ya kukaa ndani | Muungwana BLOG

Mwanaume afariki 'kufuatia kipigo cha polisi' kwa kukiuka masharti ya kukaa ndani

Kijana mmoja nchini Rwanda amefariki baada ya kupigwa na afisa wa polisi kwa kosa la kukiuka marufuku ya kutembea usiku.


Familia yake imeeleza kuwa Flavien Ngaboyamahina alikuwa anatimiza miaka 30 kesho Jumatano, alienda kumtembelea rafiki yake Mashariki mwa mji wa Kigali.


Yeye na rafiki yake walikamatwa wakati wakirejea nyumbani baada ya saa tatu usiku, muda ambao ulikuwa wa marufuku ya kutembea nje.


Jumatatu, msemaji wa polisi wa Rwanda aliiambia BBC kuwa hawezi kuchangia jambo lolote katika hilo.

“Walikuwa barabarani karibu na nyumbani kwa rafiki yake, ambapo ghafla walisikia Flavien akipiga mayowe kuwa amepigwa vibaya. Walikuwa ni polisi ,ambao waliwakamata wote wawili.” –mwanafamilia iliiambia BBC.


Bwana Ngaboyamahina alipigwa Jumamosi na alifariki Jumanne wiki iliyopita.


Taarifa zaidi kuhusu namna alivyopigwa haijafahamika bado, na wengi wanaogopa kueleza kilichotokea.


Wakati bwana Ngaboyamahina alipozikwa siku ya Alhamisi, polisi walituma mwakilishi wao na kuwaambia familia kuwa haki itatendeka, mwana familia mwingine alieleza.

Hivi karibuni Rwanda, ilisifiwa na Shirika la Afya Duniani, mkuu wa WHO Tedros Ghebreyesus alisema kuwa taifa hilo linakabiliana vizuri na janga la mlipuko wa corona.


Pia Rwanda ni miongoni mwa mataifa matatu ya Afrika ambayo yanaruhusiwa kusafiri na kuingia nchi za bara la Ulaya licha ya mlipuko wa corona.


Upinzani nchini Rwanda umelaani ukiukwaji wa haki za binadamu na matumizi ya mabavu ya maofisa wa polisi katika kukabiliana na janga la corona.


Wiki mbili zilizopita, zaidi ya watu 60,000 waliadhibiwa kwa kutovaa barakoa, kutembea usiku wakati wa marufuku ya kutembea usiku, kutokaa kwa umbali, waziri wa mambo ya ndani alieleza.


Wengi wao walikamatwa na kupelekwa katika viwanja vya mpira na majengo ya shule ambako wanalazimishwa kukaa usiku mzima au mchana wote.

Post a Comment

0 Comments