Baba amuua mwanaye kisa kuchelewa kurudi nyumbani

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linamshikilia Baba mmoja anayefahamika kwa jina la Anthony Maningu, Mkazi wa Kayenze wilayani Ilemela mkoani Mwanza kwa tuhuma za kumuua kwa kumpiga na kitu kizito kichwani mwanaye aitwae Veronica Anthony, kwa madai ya kuchelewa kurudi nyumbani.

Akizungumza hii leo Septemba 10, 2020, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Muliro Jumanne, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo, na kusema Baba huyo yupo chini ya ulinzi na uchunguzi wa tukio hilo bado unaendelea, na mwili wa mtoto huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando.

Katika tukio lingine, Kamanda Muliro amesema katika Kata ya Shibula wilayani Ilemela, Emmanuel Joseph mwenye umri wa miaka 49, aliuawa kwa kupigwa na kitu kizito utosini na ndugu yake aitwae Mussa Gabriel, baada ya kumtuhumu kumuibia simu yake yenye thamani ya Shilingi elfu Arobaini.