Kaimu Kamishna wa mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania awaasa watumishi kuongeza juhudi katika kukusanya mapato ya Serikali

 



Na Farida Saidy.

Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wanyamapori (TAWA) Bw.Mabula Misungwi Nyanda amefanya kikao na watumishi wanaosimamia eneo la mfumo ikolojia ya Ziwa Natron, Mto wa Mbu na Longido na kuwaagiza watumishi wa eneo hilo kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano kwani eneo wanalosimamia ni eneo la kimkakati katika kukusanya mapato ya Serikali.

Akizungumza katika kikao hicho kilichowakutanisha viongozi mbalimbali kutoka wizara ya maliasili na utalii Kamishna aliwaeleza watumishi kuwa uongozi unatambua changamoto zilizopo kwenye eneo hilo na kuwaasa wasikate tamaa kwa kuwa changamoto hizo zinashughulikwa.

Aidha, Kamishna pia alifafanua mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na Serikali kwa lengo la kuboresha utendaji ikiwemo Mabadiliko ya majukumu la kukusanya maduhuli ambayo yamehamishiwa kwa Mamlaka ya Mapato (TRA) pamoja na Taratibu za utekelezaji wa Jeshi USU kuanzia ngazi ya Wizara hadi kwenye Taasisi za uhifadhi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii.

Nao  baadhi ya  Watumishi waliipongeza Menejimenti ya TAWA kwa jitihada mbalimbali zinazofanywa na mamlaka hiyo ambazo zimeanza kuleta mabadiliko chanya katika utendaji wao wa kazi.

Nae  Naibu Kamishna wa Huduma za Utalii na Biashara Bw.Imani R. Nkuwi aliwapongeza watumishi wa (TAWA )kwa juhudi zao za kusimamia rasilimali za wanyamapori pamoja na changamoto zilizopo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Sheria kutoka Wizara ya Maliasili aliwaeleza watumishi kuwa kufuatia mabadiliko ya Sheria yaliyofanyika , Wizara inaandaa kanuni na miongozo mbalimbali kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa Sheria hiyo.

Kikao hicho ambacho kilihudhuriwa na Naibu Kamishna wa Huduma za Utalii na Biashara Bw. Imani R. Nkuwi, Mkurugenzi wa Sheria (DLS) Bi.Lucy Seleko kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii ,Kaimu Kamishna Msaididizi Mwandamizi Kanda ya Kaskazini Bw. Mbanjoko Peter, Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Matumizi Endelevu ya Wanyamapori Bi. Segorine Tarimo na Afisa wa Sheria kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii Bi. Happiness Salago. 

Post a Comment

0 Comments