Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye kuwasili nchini leo


Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye anatarajiwa kuwasili mkoani Kigoma hii leo Septemba 19, 2020, kwa ziara rasmi ya siku moja kufuatia mwaliko aliopewa na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Magufuli.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa kitengo cha mawasiliano serikalini, Emmanuel Buhohela, ambapo imesema kuwa mbali na kupokelewa na Rais Magufuli, Rais huyo wa Burundi pia atapokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje Profesa Palamagamba Kabudi, pamoja na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa Rais Magufuli na mgeni wake watazungumza na Watanzania hii leo katika viwanja vya Lake Tanganyika mkoani Kigoma, kabla ya kuzindua jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Kigoma, ambapo baadaye watafanya mazungumzo yao rasmi Ikulu ndogo iliyopo mkoani humo.

Ikumbukwe kuwa hii ndiyo ziara ya kwanza ya Rais Ndayishimiye nchini, tangu alipoapishwa rasmi kuwa Rais wa Burundi mapema Juni 18 mwaka huu.
 

Post a Comment

0 Comments