https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mariam Ditopile amuwashia moto Mgombea Chadema ' Wanaeneza Chuki na Ukabila' | Muungwana BLOG

Mariam Ditopile amuwashia moto Mgombea Chadema ' Wanaeneza Chuki na Ukabila'

MGOMBEA Ubunge wa Viti Maalum Wanawake Mkoa wa Dodoma CCM, Mariam Ditopile ameshiriki kampeni za chama hicho kata ya Msaada wilayani Chemba ambapo amemuombea kura Mgombea Urais wa CCM, Dk John Magufuli, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Chemba, Mohammed Monni na Diwani wa kata hiyo, Abushiri Nyori.

Akizungumza na wananchi wa Kata hiyo ya Msaada, Ditopile amesema serikali ya CCM inayoongozwa na Dk Magufuli imefanya kazi kubwa ya kuwahudumia watanzania na ndio maana kwa miaka mitano imefanikiwa kufikia uchumi wa kati, kutoa elimu bure ambayo hadi Nchi zingine zinakuja kuiga mfumo wa utoaji elimu bure, kusambaza mtandao wa lami kila Mkoa pamoja na kusambaza umeme karibu kila kijiji nchini.

Amesema Wilaya ya Chemba ni wanufaikaji wakubwa wa serikali ya Dk Magufuli ambapo ndani ya kipindi cha miaka mitano yake alipeleka kiasi cha Sh Bilioni 1.3 kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya huku pia wakipatiwa vituo vinne vya afya ambavyo vimekua msaada kwa wananchi wa Msaada na Chemba kupata huduma za afya na kuacha kusafiri umbali mrefu kwenda kutibiwa.

" Huyo mgombea Ubunge wa Chadema amekosa Sera na kwa sababu hata Chama chake hakika Ilani amebaki kuhubiri ubaguzi wa Ukabila, hawa wapinzani wamekua ni watu wanaochochea ubaguzi wa kidini na kikabila, tukiwapa nafasi watuongoze watatugawa, nani asiyejua Chemba na Kondoa ilikua Wilaya moja?

Leo tuanze kuulizana makabila yetu kweli? Huku ni kuidharau kazi kubwa ya kuunganisha umoja na mshikamano iliyofanywa na Mwalimu Nyerere, anajinadi alikua Mbunge wa Viti Maalum Dodoma, tukimuuliza kwa miaka mitano amefanya nini Chemba hadi tumpe Ubunge atatuonesha alichotupa? Tusimsikilize, mtu sahihi kwa ajili ya Chemba ni Monni peke yake," Amesema Ditopile.

Amesema mgombea Ubunge wa Chadema jimbo la Chemba kwa miaka mitano alikua akisusia vikao vya Bunge vilivyokua vikipitisha bajeti ya maslahi ya maendeleo ya Chemba huku akutumia fedha zake kuwekeza biashara zake kwenye maeneo ya nje ya Jimbo hilo.

" Anasema Chemba hakuna barabara lakini ameendesha gari kutoka Mjini kuja hapa sasa sijui alikuja kwa ungo? Miaka mitano ya Ubunge wake wa Viti Maalum hakuna la maana alilofanya Chemba zaidi ya kuhubiri ubaguzi wa kikabila na kuwagawa wananchi, angekua anaipenda Chemba angewekeza biashara zake hapa ili vijana wa hapa wapate Ajira na kuchochea uchumi lakini yeye kawekeza Mjini," Amesema Ditopile.


Amewaomba wananchi wa Kata ya Msaada kujitokeza kwa wingi Oktoba 28 kumchagua Dk Magufuli kuwa Rais kwa awamu nyingine, kumchagua Monni awe mbunge wao na Abushiri kuwa Diwani wa kata hiyo ili kwa pamoja wazungumze lugha moja ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Msaada na Chemba.

 

Post a Comment

0 Comments