Unaweza kusema ni safari ndefu ya uongozi ya mkuu wa Mkoa mpya wa Dar es Salaam, Amos Makalla.
Makalla aliyewahi kuhudumu katika idara mbalimbali za Serikali na CCM kwa nyakati tofauti leo Jumamosi Mei 15, 2021 ameteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan kushika nafasi hiyo.
Ni muda umepita jina la Makalla lilikuwa kimya masikio mwa Watanzania na hata mwaka jana alipojitokeza kuwania nafasi ya ubunge wa Mvomero, alishinda kura ya maoni ndani ya CCM lakini jina lake halikurudi.
Lakini leo Rais Samia amemteua tena kuwa mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam akichukua nafasi ya Abubakar Kunenge aliyehamishiwa Mkoa wa Pwani kuendelea na wadhifa huo.
Itakumbukwa kuwa Makalla alishawahi kushika nafasi ya katibu wa uchumi na fedha wa CCM na aliwahi kukaimu nafasi ya katibu wa umoja wa vijana wa CCM ( UVCCM).
Pia. Amewahi kuwa mbunge wa Mvomero kwa vipindi tofauti na mara ya mwisho alikuwa mbunge mwaka 2010 hadi mwaka 2015.
Makalla pia, amewahi kuwa naibu waziri wa habari enzi za utawala wa Rais mstaafu Jakaya Kikwete.
Aliwahi kuwa mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro kisha kuhamishiwa Mkoa wa Mbeya kabla ya kuhamishiwa Mkoa wa Katavi.
Mei 14, 2019 Hayati John Magufuli alitengua uteuzi wake akiwa mkoani Katavi.
Leo Makalla ameanza kuandika historia nyingine ya kwa nafasi ileile aliyekuwa nayo mkoani Katavi kabla ya kutumbuliwa na Magufuli.
0 Comments