AFCON: Taharuki kufuatia mchuano kati ya Mali na Tunisia

 


Hali ya taharuki ilitanda Jumatano jioni kwenye michuano ya kombe la Afrika, AFCON, nchini Cameroon, baada ya Mali kuicharaza Tunisia kwenye mechi iliyojawa na mivutano kufuatia madai kwamba refa alipiga kipenga kabla ya dakila 90 kumalizika. 


Tukio hilo nusra lifunike ushindi wa Mali wa 1 kwa nonge wakati Gambia na Ivory Coast pia wakipata ushindi wa goli moja kila mmoja wakati wa kutamatisha raundi ya kwanza ya makundi.


Shirika la habari la AFP liliripoti kwamba hasira zilipanda baada ya refa kutoka Zambia Janny Sikazwe kupiga filimbi ya mwisho wakati ikiwa dakika ya 89 na sekunde 42, hatua iliyopelekea Tunisia kuvunjika moyo wakati wakijitahidi walau kupata goli moja dhidi ya Mali ambayo ilikuwa na wachezaji 10 pekee.


Hali ya sintofahamu ilijitokeza zaidi wakati kocha wa Mali Mohamed Magassouba alipokuwa akizungumza na wanahabari kufuatia ushindi wa timu yake, lakini kabla ya kumaliza afisa mmoja akamkatiza na kusema kwamba mechi ingeendelea kwa dakika zingine 3.


Baada ya hapo timu ya Mali ilirejea uwanjani lakini ile ya Tunisia haukurudi na kwa hivyo Mali ikatangazwa rasmi kuwa mshindi wa mechi hiyo.


Haijabainika iwapo hatua ya Tunisia ya kutorejea uwanjani itapelekea kuchuliwa hatua za kinidhamu na shirikisho la soka la Afrika.

Post a Comment

0 Comments