Ndejembi awataka Wakuu wa Idara na Vitengo kutenda haki kwa watumishi wa chini

NAIBU Waziri Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Deo Ndejembi amewataka Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala kuhakikisha wanasimamia mambo manne ambayo ni Haki, Utunzaji wa Siri za Serikali, Ubunifu na Kutunza Vipaji sambamba na kupima ubora wa utendaji kazi wa watumishi nchini.

Ndejembi ametoa kauli hiyo jijini Dodoma wakati alipokua akizungumza kwenye kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Utumishi wa Umma.

" Ofisi ya Rais Utumishi tumekua tukipokea malalamiko kutoka kwa watumishi wetu kwamba nyinyi Wakuu wa Idara na Vitengo hamshughulikii changamoto zao, niwaase kutenda haki na kumthamini kila mtumishi aliye chini yetu, lakini pia niwaase kujifunza kutunza siri za serikali hasa pale mnapoona jambo linafanyiwa upekuzi.

Jambo lingine ni kuongeza ubunifu kazini, epukeni kuwa walewale kila siku, Kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma ziko wazi lakini hatumzuii mtu kuonesha kipaji chake na kuwa mbunifu ili kuongeza ubora wa kazi zake," Amesema Ndejembi.

Amewataka Wakuu hao wa Idara na Vitengo kuhakikisha pia wanapima utendaji kazi wa watumishi kwani litakua jambo la aibu kuona mtumishi wa umma anafanya kazi chini ya ubora unaotakiwa ilihali Serikali imeonesha kujali maslahi yao.

" Watumishi wa umma tuna deni kubwa kwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan, tayari yeye ameonesha kwa vitendo kuwajali watumishi ambapo ameongeza mshahara kwa asilimia 23 kama hiyo haitoshi tayari ametoa kibali cha kuongeza posho za watumishi, tumlipe Rais wetu kwa kufanya kazi kwa bidii," Amesema Ndejembi.

 

Post a Comment

0 Comments