Na Ahmad Mmow, Nachingwea.
Chama kikuu cha ushirika cha RUNALI, mkoani Lindi, leo kimefanikiwa kuuza kilo zote 3,628,708 zilizopo kwenye maghala makuu kupitia mnada wa kwanza wa zao hilo kwa msimu wa 2022/2023.
Kwenye mnada huo uliofanyika mjini Nachingwea katika viwanja vya ofisi kuu ya chama hicho ulinunuliwa kwa bei ya juu kwa kila kilo moja kwa shilingi 3,036.00. Ambapo bei ya chini ilikuwa shilingi 2,955 kwa kila kilo moja.
Kwamujibu wa meneja mkuu wa RUNALI, Jahida Hassan kampuni 22 zilijitokeza kuomba kununua ufuta huo uliopo katika maghala ya Lipande( Ruangwa), Nachingwea Export (Nachingwea), Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea(Nachingwea), Hassan Mpako na Umoja (Liwale).
Alibainisha kwamba kwamba ghala la Nachingwea Nachingwea Export lina 354,921, Halmashauri ya Nachingwea kilo 630,389, Lindi farmers kilo 244,721, Umoja tani 440,602. Ambapo ghala la Hassan Mpako lina kilo 622,656.
Wakizungumza baada ya wakulima kuridhia kuuza ufuta huo kwabei hizo, katibu tawala wa wilaya ya Nachingwea, Omari Mwanga ambae alimwakilisha mkuu wa wilaya ya Nachingwea aliwataka wanunuzi waliofanikiwa kununua ufuta huo waharakishe malipo ili wakulima walipwe haraka.
Nae mwenyekiti wa RUNALI, Audax Mpunga alitoa wito kwa wakulima wadhibiti ubora wa ufuta ili bei ziendelee kupanda na kuwa imara.
Aidha Mpunga aliwaasa wakulima wa korosho wilayani Nachingwea wapalilie mashamba yao ili isiungue moto. Kwani iwapo itaungua watakuwa wamemuangusha Rais Samia Suluhu Hassan ambae serikali anayoongoza inawapa viuatilifu na pembejeo bila malipo.
Mnada huo ni wanne kwa mkoa wa Lindi kwa msimu wa 2022/2023 na wakwanza kwa RUNALI. Kwani chama kikuu cha ushirika cha Lindi Mwambao kimefanya minada mitatu.
0 Comments