Afisa Madini mkazi wa Mkoa wa Dodoma awakaribisha wawekezaji Dodoma

 


Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma Mhandisi Nchagwa Marwa amewakaribisha wawekezaji wa madini kuwekeza kwenye shughuli za uchimbaji wa madini kutokana na mkoa huo kuwa na madini ya aina nyingi ikiwemo ya viwanda, ujenzi, vito na metali na kusisitiza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji.

Mhandisi Marwa ameyasema hayo leo Agosti 05, 2022 kwenye  maonesho ya Nane Nane ya Kanda ya Kati yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.

 Amesema kuwa  Serikali kupitia Tume ya Madini imeweka mazingira rafiki ikiwa ni pamoja na utoaji wa leseni za uchimbaji na biashara ya madini kwa wakati ili kuwezesha shughuli za uchimbaji na biashara ya madini kufanyika kwa tija.

 Akizungumzia biashara ya madini katika mkoa wa Dodoma,  ameeleza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini imefungua masoko ya madini nchini na kusisitiza kuwa ofisi yake imejipanga kutoa  leseni za biashara na  vibali kwa ajili ya kusafirisha madini kwa haraka ikiwa ni mkakati wa kurahisisha shughuli za biashara ya madini.

 Katika hatua nyingine amewataka wachimbaji wa madini kuzingatia matakwa ya  Sheria ya  Madini ikiwemo kulipa ada za mwaka za leseni kwa wakati ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kutozwa faini na kufutiwa leseni hizo.

 

Post a Comment

0 Comments