Kenya: Mili ya maafisa 8 wa usalama waliouawa na majambazi Turkana yapelekwa Nairobi

 


Mili ya maafisa wa polisi waliouawa katika shambulio la majambazi lililofanyika Jumamosi katika eneo la  Turkana Mashariki, nchini Kenya, iliwasili mjini Nairobi Jumapili jioni.


Maafisa wanane wa polisi waliuawa katika shambulizi hilo, pamoja na Chifu wa eneo hilo na mwanamke mmoja.


Waathiriwa walivamiwa walipokuwa wakifuata genge la majambazi waliokuwa wamejihami kwa silaha nzito, wanaoshukiwa kutoka kaunti jirani ya Baringo.


Kamanda wa Polisi wa Turkana Samuel Ndanyi alithibitisha kisa hicho akisema waathiriwa waliviziwa katika eneo la Namariat karibu na kijiji cha Kakiteitei.


Rais wa Kenya William Ruto amelaani sahmbulizi hilo, na kuahidi kwamba serikali itachukua hatua kali dhidi ya waliolitekeleza.


Wizi wa mifugo au ugomvi kuhusu malisho, na vyanzo vya maji ni jambo la kawaida kati ya jamii za wafugaji wa ng'ombe kaskazini mwa Kenya. Mnamo Novemba 2012, zaidi ya polisi 40 waliuawa katika shambulizi la kuvizia walipokuwa wakiwafuata wezi wa mifugo huko Baragoi, wilaya ya mbali kaskazini mwa Kenya.

Post a Comment

0 Comments